Na Mwandishi Wetu, Rorya.
Mkurugenzi wa shirika lisilo la Kiserikali la Hope for Girls and Women in Tanzania linalojishughulisha na kupambana na ukatili wa Kijinsia Mkoani Mara Rhobi Samwelly, amewataka Wanawake kuendelea kuzitumia vyema fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwa ni pamoja na mafunzo ya ujasiriamali na mikopo nafuu inayotolewa na Serikali kusudi waweze kujiletea maendeleo.
Ameyasema hayo Machi 6, 2026, alipokuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya Wanawake Wilayani Rorya Mkoani Mara.
Maadhimisho hayo yamefanyika kata ya Koryo katika uwanja wa Shule ya Msingi utegi na kuhudhuriwa na makundi mbalimbali ya Wanawake kutoka Sekta binafsi, taasisi za umma, serikalini pamoja na Wananchi Wilayani humo.
Ambapo kauli mbiu ya mwaka huu inasema 'Haki kwa Wanawake na Wasichana, Msingi wa maendeleo jumuishi kufikia Dira 2050'
Rhobi amesema, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Hassan imeendelea Kutoa fursa ya mikopo nafuu kwa wanawake, hivyo ni muhimu wakachangamkia fursa hiyo ili waweze kujikwamua kiuchumi kwa kufanya shughuli za biashara na ujasiriamali.
Pia, amewataka wanawake Wilayani humo, kutumia siku hiyo kujitathmini na kuimarisha malezi bora kwa watoto wao kwani wana nafasi nzuri kuimarisha malezi, makuzi sambamba na kusimamia maadili mema yatakayowasaidia watoto kukua katika mazingira salama na yenye heshima.
Pia, amesisitiza wanawake kujiepusha na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, akieleza kuwa ukatili unaathiri maendeleo ya watoto kimwili, kiakili na kisaikolojia. Huku akihimiza wazazi na walezi kuwalinda watoto na kuwapa malezi yenye upendo wakizingatia haki za watoto ili kuwasaidia kufikia ndoto zao za baadaye.
"Wanawake tukijiimarisha kiuchumi tutaweza kusaidia familia zetu, kuwapatia watoto mahitaji muhimu na kuchangia maendeleo ya jamii na Taifa letu kwa ujumla."amesema Rhobi.
Akisoma risala ya Wanawake wa Wilaya ya Rorya Lilian Fransisco ambaye ni Mratibu wa Dawati la Wanawake Wilaya ya Rorya amesema anaipongeza serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuwathamini Wanawake na kutatua changamoto zao mbalimbali.



