Na Mwandishi Wetu, Butiama.
TAASISI ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) imepongeza juhudi zinazofanywa na Shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika kupambana na ukatili wa kijinsia na kusaidia watoto wa kike kutimiza ndoto zao Mkoani Mara.
Pongezi hizo zimetolewa Julai 10, 2026 na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Utamaduni, Makongamano na Utalii, Hashimu Omary, alipotembelea Kituo cha Nyumba Salama Butiama. Akiwa pamoja na viongozi mbalimbali wa SMAUJATA kutoka ngazi ya Kanda na Mkoa wa Mara.
Kituo cha Nyumba Salama Butiama kinamilikiwa na shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania. Ambapo limeendelea kupambana na ukatili wa kijinsia Mkoani Mara kwa kutoa elimu ya ukatili kwa jamii, makongamano, kutoa msaada kwa wasichana wanaokimbia ukeketaji na ndoa za utotoni kwa lengo la kuiwezesha jamii kuachana na vitendo hivyo.
Akizungumza na wasichana waliopo kituoni hapo, ambao wamepata hifadhi baada ya kukimbia vitendo mbalimbali vya ukatili ikiwemo ukeketaji na ndoa za utotoni kutoka katika familia zao, Hashimu amewataka kusoma kwa bidii na kusimamia ndoto zao kwani serikali imeweka mazingira bora kwa kila mtoto kupata elimu.
"Nimpongeze Mkurugenzi wa shirika hili, Rhobi Samwelly, kwa maono yake ya kuanzisha Nyumba Salama hii ambayo imekuwa msaada kwenu. Mnapata hifadhi, mnaendelezwa kielimu, na mnapatiwa mahitaji mbalimbali mkiwa hapa. Someni kwa bidii ili muje kusaidia jamii katika nyanja mbalimbali na pia muendelee kuwa mabalozi wa kupinga ukatili na kuchochea maendeleo," amesema Hashimu.
Ameongeza kuwa, SMAUJATA itaendelea kushirikiana na Shirika la Hope, wadau mbalimbali pamoja na Serikali katika kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili. Lengo ni kusukuma mbele juhudi za maendeleo na usawa katika jamii kwa manufaa endelevu.
Kwa upande wake, Afisa Mwelimishaji Jamii wa shirika hilo, Emmanuel Good Luck, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Rhobi Samwelly, ameipongeza SMAUJATA kwa kuwatembelea wasichana hao. Amesema, ziara hiyo imewatia moyo wasichana hao na kuwakumbusha kuwa hawako peke yao.
"Tunawashukuru kwa kuwapa ushauri na kuwatia moyo ili wasijione wapweke. Wametambua kuna watu nyuma yao wanaowaombea kwa Mungu baraka na heri ili wahakikishe wanatimiza ndoto zao, kwani," amesema Good Luck.
Pia, Goodluck amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi, kwa kuendelea kukemea vikali vitendo vya ukatili wa Kijinsia na kuhamasisha mabadiliko chanya kwa wananchi ili kuachana na mila potofu na zenye madhara kwa wasichana jambo ambalo limeendelea kuwa na manufaa katika juhudi za kutokomeza ukatili mkoani humo.




