Jinsi Mazoea Hatarishi ya Uvuvi na Vifaa Duni vya Usalama Vinavyowaweka Wavuvi Katika Hatari ya Kupoteza Maisha

0


 


Na Emmanuel Chibasa

Ni jambo la kawaida ukifika  katika baadhi ya maeneo ya fukwe na mialo ya Ziwa Victoria nyakati za jioni na kukuta wavuvi wamekusanyika kwa makundi, wakipakia nyavu zao na vitendea kazi vingingine kwenye mitumbwi kabla ya kuanza safari ya usiku kutafuta samaki na dagaa.

Baadhi yao huonekana wamevaa life jackets huku  wengine wakiwa hawajavaa lakini kwa wengi, hilo si chaguo la uhakika wa usalama ni chaguo la kuendelea kuishi kama anavyoeleza Josiah Sabato

“Tunavaa hizi life jacket lakini sisi tunaziona hazina ubora kabisa sijui kwa kwa sababu ya bei tunayonunua ni ya kiwango cha chini au sehemu  zinapotengenezwa wanaengeneza chini ya kiwango labda viongozi huko ndio watuambie Kwa Nini zipo hivi sababu ikitokea mtu amezama  itamsaidia kwa muda mfupi sana  tofauti na watu huko nje wanavyouchukulia ” Anasema Josia 

Lakini licha ya hofu hiyo, hakuna anayebaki nyumbani. Kila mtu ana sababu moja inayofanana.

“Tunajua watu wanazama lakini tukikaa nyumbani familia itakula nini? Huku sisi ndio sehemu tunapata pesa ya chakula, ada za watoto na mahitaji mengine"

Licha ya changamoto hizo lakini hakuna anayebaki nyumbani kama ilivyo kwa  Josia, ambaye anaeleza wazi kwamba Ziwa Victoria sio tu ni sehemu  ya kupata mazao ya samaki, bali pia ni sehemu ya kujipatia riziki katika kukuza uchumi binafsi na taifa kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Sekta ya Uvuvi imeendelea kuwa nguzo muhimu katika uchumi wa taifa, ikichangia asilimia 1.6 ya Pato la Taifa (GDP) mwaka 2024 na kukua kwa asilimia 2.3.

Sekta hiyo pia inakadiriwa kunufaisha zaidi ya Watanzania milioni 6 katika mnyororo wa thamani, kuanzia uvuvi, usindikaji, biashara hadi usafirishaji.

Hata hivyo nyuma ya takwimu hizi za mafanikio ya kiuchumi, kuna simulizi tofauti kabisa katika mwambao wa Ziwa Victoria simulizi ya maisha yanayoishi hatarini kila siku.

 Maisha ya Hatari Ziwani

Adam Maingu (58), mkazi wa Nyakato Mlimani Manispaa ya Musoma anajishughulisha na uvuvi wa dagaa katika Ziwa Victoria, anasema kazi hiyo imekuwa sehemu ya maisha yake ya kila siku. Anaeleza kuwa kwa wiki huenda ziwani mara sita au hata saba kutegemeana na hali ya hewa na mara nyingine hurudi mikono mitupu lakini hana namna nyingine ya kujipatia kipato cha kuendesha maisha ya familia yake.

Anasema changamoto kubwa inayomkabili katika kazi yake hiyo ni ukosefu wa life jacket kutokana na gharama kuwa juu, hali inayowafanya baadhi ya wavuvi pia kutegemea vifaa vilivyopo kwenye mtumbwi ambavyo mara nyingi havitoshi.

Anakumbuka tukio la hatari siku moja walipokutana na upepo mkali na mawimbi makubwa yaliyotokea ghafla usiku wakiwa ziwani, ambapo mtumbwi wao ulianza kujaa maji kidogo kidogo na walilazimika kupambana kwa muda mrefu kabla ya kufika salama ufukweni.

“ licha ya hatari hizo, uvuvi bado ni tegemeo lake kuu la maisha kwani ndiyo unaomwezesha kuhudumia familia, kulipa ada za watoto na kugharamia mahitaji ya kila siku, hivyo anaendelea kufanya kazi hiyo huku akichukua tahadhari kadiri iwezekanavyo.’Amesema Adam

Ajali Zinavyo badilisha Maisha

Idd Magere (42), mkazi wa Machinjioni kata ya Rwamlimi Manispaa ya Musoma na mvuvi katika Ziwa Victoria, anasimulia tukio la hatari lililobadilisha mtazamo wake kuhusu usalama majini. Anasema akiwa pamoja na wenzake ziwani hali ya hewa ilibadilika ghafla, upepo mkali ukaanza kuvuma na mawimbi makubwa. Katika hali hiyo, mtumbwi mmoja uliokuwa karibu yao ulipigwa na mawimbi na kupinduka, na waliokuwa ndani yake walijikuta wakipambana kuogelea lakini si wote waliweza kujiokoa.

Anasema eneo la ajali lilikuwa mbali na nchi kavu na hakukuwa na boti ya uokoaji karibu jambo lililofanya juhudi za msaada kuwa ngumu zaidi. Waliopata ajali hawakuwa wamevaa life jacket hivyo walichoka haraka walipojaribu kuogelea. Anasema wao walijaribu kusaidia kwa kutumia mitumbwi wao, lakini uwezo wake ulikuwa mdogo na kuchelewa kuwafika kuliathiri uokoaji.

“Tukio hilo lilinifundisha kubadilika nikiwa majini, siku hizi nangalia hali ya hewa kabla ya safari na pale ninapoona dalili za upepo mkali au mvua  huahirisha safari licha ya changamoto za kipato na kutumia mtumbwi wa kasia, kuchukua tahadhari na kutumia life jackets pale inapowezekana ni hatua muhimu ya kuokoa maisha ingawa hizi life jacket tunazovaa hata ukizama nusu saa tu unaenda nayo chini.’Ameongeza Idd

Uelewa na Tabia za Wavuvi

Damas Leonard mvuvi katika eneo la Mwisenge na mkazi wa Kamnyonge Manispaa ya Musoma anasema wavuvi wengi katika mwambao wa Ziwa Victoria hutegemea zaidi uzoefu wao wa muda mrefu kuliko elimu rasmi ya usalama majini. Anasema hali hiyo imekuwa changamoto kwa sababu uzoefu pekee hauwezi kutabiri mabadiliko ya ghafla ya hali ya hewa ziwani jambo linaloweka maisha ya wavuvi hatarini hasa wanapoingia majini bila tahadhari za mwongozo wa kitaalamu.

Naye Zakayo Mauma ambaye pia ni mvuni na mkazi wa mkinyerero manispaa ya Musoma akieleza kuwa, licha ya taarifa za hali ya hewa kupatikana kupitia vyombo vya habari, bado baadhi ya wavuvi huzipuuza na kuendelea na safari zao kama kawaida. Anasema tabia hiyo inachochewa na uhitaji wa kipato cha haraka, lakini imekuwa ikisababisha ajali zinazoweza kuzuilika, hasa pale hali ya hewa inapobadilika ghafla wakati wavuvi wakiwa tayari ziwani.

Gharama ya Vitendea Kazi na Hali ya Usalama

Bahati Kabasa mmiliki wa mtumbwi wa mvuvi wa dagaa katika eneo la Mwisenge Manispaa ya Musoma, anasema changamoto kubwa inayowakabili wamiliki wa mitumbwi na wavuvi ni bei kubwa na upatikanaji mdogo wa life jackets zenye ubora.

“Hali ya upatikanaji wa samaki na dagaa kwa sasa imepungua sana na  inatulazimu wavuvi wetu kwenda umbali mrefu zaidi ziwani kutafuta riziki lakini hata hivyo mavuno bado ni madogo na muda mwingine wanakosa kabisa lakini unakuta tunatumia gharama kubwa za uendeshaji hali inayopelekea kushindwa kumudu kununua life jackets zenye ubora.” Amesema Bahati

Anasema kutokana na kipato kupungua wavuvi wengi pamoja na wamiliki wa mitumbwi hushindwa kumudu kununua life jackets zenye ubora wa juu. 

Bahati anasema baadhi ya life jackets zinazopatikana sokoni huuzwa kati ya shilingi 20,000 hadi 25,000 lakini hazina uwezo wa kutosha wa kuokoa maisha ambapo ametoa wito kwa serikali kuangalia ubora wa bidhaa hizo  katika maduka lakini pia kupunguza gharama au kutoa ruzuku, akisema endapo life jackets bora zingepatikana kwa bei ya chini wavuvi wengi wangeweza kumudu na kuongeza usalama wao majini.

Robinson Wangaso ni mjumbe wa kamati ya maafa na habari wa Tanzania Red Cross Society mkoa wa Mara, anasema sababu kuu zinazochangia matukio ya watu kuzama katika Ziwa Victoria ni pamoja na kutotumia vifaa vya kuokoa maisha kama life jackets, matumizi ya vyombo visivyo salama au vilivyochakaa, pamoja na kupakia abiria na mizigo kupita uwezo wa vyombo hivyo. Pia anasema baadhi ya wavuvi na wasafiri huendelea na safari hata wakati wa upepo mkali na mawimbi makubwa jambo linaloongeza hatari ya ajali zinazoweza kuzuilika.

Anasema makundi yaliyo katika hatari zaidi ni wavuvi wadogo, wasafiri wa kila siku wanaotumia usafiri wa majini, watoto wanaoishi karibu na fukwe za Ziwa Victoria pamoja na wananchi wasiokuwa na ujuzi wa kuogelea. Hali hii inaonyesha kuwa changamoto ya kuzama si ya kundi moja pekee, bali ni ya kijamii na kiuchumi inayogusa maisha ya watu wengi, hivyo elimu ya usalama majini na matumizi ya vifaa vya kujikinga ni muhimu zaidi.

“Tanzania Red Cross Society imekuwa ikiendesha kampeni za uhamasishaji katika mwambao wa Ziwa Victoria, ikisisitiza matumizi ya life jackets, kuzingatia utabiri wa hali ya hewa kabla ya safari na kufuata taratibu za usalama majini. Pia tumekuwa tukitoa mafunzo ya huduma ya kwanza na mbinu za msingi za uokoaji kwa jamii ili kuongeza uwezo wa kutoa msaada wa haraka pindi ajali zinapotokea.” Amesema Wangaso

Ameongeza kuwa mbali na kuendesha kampeni hizo lakini bado kuna changamoto upungufu wa vifaa vya kisasa vya uokoaji kama boti za uokoaji, vifaa vya mawasiliano na huduma ya kwanza, pamoja na umbali wa baadhi ya maeneo ya ajali unaochelewesha uokoaji ambapo anasisitiza kuwa suluhisho linahitaji ushirikiano wa serikali, Red Cross na jamii kwa pamoja ikiwemo utekelezaji wa sheria za usalama majini, ukaguzi wa vyombo vya usafiri na kuongeza vituo vya uokoaji katika maeneo hatarishi.

Kwa mujibu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), zaidi ya wavuvi 32,000 hupoteza maisha kila mwaka duniani kutokana na ajali mbalimbali zinazotokea majini. Shirika hilo linaeleza kuwa idadi hiyo huenda ikawa ndogo kuliko hali halisi kutokana na changamoto za kuripoti vifo vinavyotokea baharini na maziwani.

FAO inaeleza kuwa karibu watu milioni 60 duniani wanajishughulisha na sekta ya uvuvi na ufugaji wa samaki, huku wengi wao wakiwa katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati. Wanawake wanakadiriwa kuunda asilimia 21 ya nguvu kazi katika sekta hiyo, na zaidi ya asilimia 40 ya samaki wanaovuliwa duniani hutokana na uvuvi mdogo. Pamoja na mchango huo mkubwa katika usalama wa chakula na uchumi, hatari ya kuzama majini imeendelea kuwa moja ya vihatarishi vikubwa vinavyowakabili wavuvi katika shughuli zao za kila siku.

Pengo la Sera na Uhalisia

Mujura Maingu ni Afisa mradi wa Lake Victoria Drowning Prevention Project (LVDPP) mkoa wa Mara unaotekelezwa na shirika la Environmental Management and Economic Development Organization (EMEDO).

Amesema ajali nyingi za majini hazizungumzwi sana kwa sababu ni suala la kisera na kwa muda mrefu hakuna sera mahususi inayolenga moja kwa moja usalama wa maisha ya watu majini. Anasema hata katika Sera ya Uvuvi, suala la usalama wa watumiaji bado halipewi uzito wa kutosha.

Amesema Sera zilizopo zinajikita zaidi kwenye masuala ya uzalishaji, mapato, usimamizi wa rasilimali za uvuvi na tozo, lakini hazijazingatia kwa kina usalama wa watu wanaotumia maji kama sehemu ya maisha yao ya kila siku. Hii inaleta pengo kubwa kati ya uhalisia na mipango ya kitaifa.

Ameeleza kuwa utafiti unaonyesha makundi yaliyo hatarini zaidi ni wavuvi wanaokwenda ziwani kuvua, wasafiri wanaotumia usafiri wa majini, pamoja na wananchi wanaotumia ziwa kwa shughuli za kawaida kama kufua au kuoga, wakiwemo watoto na wanawake.

“ili kupunguza ajali za majini hatua ya kwanza ni elimu ya uelewa kwa jamii, kwa sababu watu wengi wamekuwa wakichukulia hatari za ziwani kama jambo la kawaida licha ya vifo vinavyoendelea kutokea.

Picha ya mkufunzi na wavuvi wakipewa mafunzo ya usalama majini pamoja na uokoaji yaliyotolewa na shirika la EMEDO Tanzania katika Mwalo wa Busekera Mkoani Mara(Picha kwa hisani ya EMEDO Tanzania)

Kupitia mradi wetu tumefanikiwa kuboresha mwitikio wa jamii katika kutoa taarifa za ajali ambapo awali wananchi walikuwa wazito kutoa taarifa, lakini sasa taarifa hutolewa haraka kwa viongozi na timu za uokoaji.

Changamoto nyingine tulioibaini katika utafiti wetu wavuvi walieleza kuwa mitumbwi inayotumika sasa haina uwezo wa kuelea vizuri kama ilivyokuwa zamani kutokana na na aina za mbao wanazotumia kutengeneza, tofauti na mitumbwi ya zamani iliyokuwa na uwezo wa kumsaidia mtu kubaki juu ya maji hata baada ya ajali kwa sasa mitumbwi mingi hutengenezwa kwa mbao duni na wakati mwingine inapozama huishia kuzama kabisa hadi kwenye tope jambo linaloongeza hatari ya vifo.” Amesema Maingu

Ameongeza kuwa kupitia mradi huo wamehamasisha matumizi ya life jackets kama suluhisho la haraka  pamoja na ukarabati wa vyombo vya usafiri majini ili kupunguza ajali zinazoweza kuzuilika lakini hata hivyo anasema changamoto kubwa bado ni gharama ya life jackets, ambapo sheria inamtaka mmiliki wa chombo kuwanunulia wafanyakazi wake, lakini wamiliki wengi wanasema kipato ni kidogo na hawawezi kumudu.

Picha ya wakufunzi na wavuvi wakipewa mafunzo ya usalama majini pamoja na uokoaji yaliyotolewa na shirika la EMEDO Tanzania katika Mwalo wa Busekera Mkoani Mara(Picha kwa hisani ya EMEDO Tanzania)

Aidha amesema mradi huo umetengeneza life jackets 500 na kuzipunguza bei kutokana na kutengenezwa kwa ruzuku kutoka shilingi 70,000 hadi 40,000, lakini bado wavuvi wengi wanashindwa kununua na badala yake huchagua zile za bei nafuu ambazo hazina uwezo wa kuokoa maisha kwa muda mrefu.

Taasisi ya Environmental Management and Economic Development Organization (EMEDO) kwa kushirikiana na  Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO),zimekua zikishirikiana kutekeleza juhudi za kuongeza uelewa wa jamii na kujenga uwezo wa wananchi katika kuzuia vifo vinavyotokana na ajali za kuzama katika Ziwa Victoria. 

Ushirikiano huo unalenga kuimarisha elimu ya usalama majini na kukuza ujuzi utakaosaidia kuokoa maisha ya wavuvi na watumiaji wengine wa ziwa hilo lenye ukubwa wa zaidi ya kilomita za mraba 68,000, na kutegemewa na wavuvi zaidi ya 100,000  kama chanzo kikuu cha maisha yao. Hata hivyo, FAO  linaonya kuwa wavuvi pamoja na jamii zinazozunguka ziwa hilo wanaendelea kuwa katika hatari kubwa ya kupoteza maisha kutokana na ajali za kuzama majini


Je Upi Mkakati wa Serikali katika Huduma za Utafutaji na Uokozi

Wakati wavuvi na wadau wa maendeleo wakieleza changangamo za usalama majini katika Ziwa Victoria  Serikali kwa upande wake imesema itaendelea kuwekeza katika sekta ya usafiri wa majini na kuimarisha huduma za utafutaji na uokozi kama sehemu ya juhudi za kulinda maisha ya wananchi, kuongeza usalama wa usafiri wa majini na kuchochea ukuaji wa uchumi wa buluu.

Akizungumza tarehe 25 Juni 2026 wakati alipotembelea Boti ya Utafutaji na Uokozi ya Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) katika Bandari ya Kigoma, ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani, Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa alisema serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu, vifaa na vyombo vya kisasa vya uokozi ili kuboresha usalama wa watu wanaotumia usafiri wa majini.


Picha ya Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa Akizungumza tarehe 25 Juni 2026 wakati alipotembelea Boti ya Utafutaji na Uokozi ya Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) katika Bandari ya Kigoma(Picha kwa hisani ya TASAC)

Prof. Mbarawa alisema TASAC imeendelea kutekeleza maelekezo ya serikali kwa kusimamia ununuzi wa boti za kisasa za utafutaji na uokozi zilizogharimu zaidi ya shilingi bilioni mbili hatua iliyoongeza uwezo wa kukabiliana na dharura katika maeneo ya maziwa na bahari huku akisisitiza kuwa, kuongezeka kwa shughuli za usafiri na biashara kupitia maji kunahitaji mifumo imara ya uokoaji na usimamizi wa usalama ili kupunguza ajali na kulinda maisha ya wananchi, huku uwekezaji huo ukiwa sehemu ya mkakati mpana wa kuimarisha uchumi wa buluu nchini.

Picha ya moja ya boti za kisasa za utafutaji na uokozi zilizonunuliwa na serikali zenye uwezo wa kukabiliana na dharura katika maeneo ya maziwa na bahari(Picha kwa hisani ya TASAC)

Lembris Machungwa ni  Afisa Uvuvi wa Manispaa ya Musoma anasema moja ya changamoto kubwa inayochangia ajali za majini ni baadhi ya wavuvi kutovaa life jackets licha ya kufahamu umuhimu wake.

 Anasema hali hiyo inatokana na mazoea ya muda mrefu, kwani kwa miaka mingi wavuvi walikuwa wakifanya shughuli zao bila kutumia vifaa hivyo vya usalama.

“Kutokana na utamaduni huo imekuwa vigumu kwa baadhi yao kubadili tabia na kuanza kuvaa life jackets kila wanapoingia ziwani na pia  kiwango kidogo cha uelewa kuhusu usalama majini na umuhimu wa kuzingatia sheria na kanuni zilizowekwa kimeendelea kuchangia baadhi ya wavuvi kuvunja taratibu za usalama, hivyo kuongeza hatari ya ajali.” Amesema Machungwa

Machungwa anasema Ofisi ya Uvuvi ya Manispaa ya Musoma imekuwa ikiendesha vikao vya kila robo mwaka na wadau wa sekta ya uvuvi, ambapo pamoja na masuala ya maendeleo ya sekta hiyo, ajenda za usalama majini hupewa kipaumbele kwa kutoa elimu na kuhamasisha matumizi ya vifaa vya kujikinga.

Anatoa wito kwa wavuvi kuhakikisha wanavaa life jackets kila wanapoingia ziwani, kutumia vyombo vinavyokidhi viwango vya usalama na kuzingatia taarifa za hali ya hewa kabla ya safari, akisisitiza kuwa kuchukua tahadhari ni hatua muhimu ya kulinda maisha na kupunguza ajali zinazoweza kuzuilika.










Chapisha Maoni

0 Maoni
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Chapisha Maoni (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top