Na
Emmanuel Chibasa
Jane
Magembe mkazi wa Mwisenge Manispaa ya Musoma, alikuwa ameamua kuachana na
matumizi ya mkaa na kuhamia gesi ya kupikia ili kupunguza gharama na kulinda afya
ya familia yake. Hata hivyo amejikuta
akijiuliza swali moja kubwa kwamba kwa nini gesi anayoinunua wakati mwingine
inawahi kuisha na haidumu kama ilivyokuwa awali?
"Nilikuwa
naagiza gesi kwa boda boda kama kawaida lakini kuna wakati mtungi haukai hata
mwezi mmoja umeisha. Nilipojaribu kuuliza wauzaji madukani walidai hata wao
hawaelewi sababu wakisema hata wao wanachukua kutoka kwa wasambazaji ikiwa hivyo," Anasema Jane.
Malalamiko
ya Jane si ya pekee. Monica Edward wa eneo la Mtakuja naye anasema watumiaji wa gesi kupikia wamekuwa wakikumbana na hali hiyo kwa kununua bidhaa ambayo hawawezi
kuthibitisha ujazo wake kwa macho na maduka mengi wanatoa huduma hiyo bila ya mizani.
"Changamoto
ni kwamba unanunua au unapoenda kujaza mtungi wa gesi lakini huwezi kujua kama umejazwa kikamilifu.
Maduka mengi ya mtaani hayana mizani. Bei za gesi zimepanda lakini bado
tunaamua kutumia gesi inasikitisha kuona wakati mwingine gesi inaisha haraka
bila sababu za msingi. Serikali inapaswa kufanya uchunguzi ili tujue nani
anatuchakachua," Anasema Monica.
Kwa
Daniel Arobogast, suluhisho ni kuweka mfumo wa lazima wa kupima mitungi yote ya
gesi mbele ya mteja.
"Kama
EWURA wamegundua changamoto hii ni muhimu wachukue hatua haraka. Kila
mfanyabiashara wa gesi anatakiwa kuwa na mzani wa kupima mtungi wakati wa kuuza
au kujaza. Watakaokiuka utaratibu huo wachukuliwe hatua kali za kisheria,"
Anasema.
Tahadhari ya EWURA Kuhusu Biashara Haramu ya Mitungi ya Gesi
Mamlaka
ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Ziwa inaeleza kuwepo kwa baadhi ya wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu wanaojihusisha na
biashara haramu ya mitungi ya gesi ya kupikia.
Akizungumza
na waandishi wa habari mkoani Mara katika ukumbi wa Mwembeni Complex wakati wa
mafunzo ya siku moja kuhusu majukumu, mafanikio, changamoto na mikakati ya
EWURA katika sekta za nishati na maji, Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa, Nyirabu
Musira, amesema mamlaka hiyo imebaini baadhi ya wafanyabiashara wakihamisha
gesi kutoka mitungi mikubwa kwenda mitungi midogo kinyume cha sheria.
Amesema
vitendo hivyo husababisha baadhi ya mitungi kuwa na ujazo usio sahihi na hivyo
kuchangia malalamiko kutoka kwa wananchi.
"Tunafahamu
kuwa kuna watu wanafanya biashara haramu ya mitungi ya gesi kwa kuhamisha gesi
kutoka mitungi mikubwa kwenda mitungi midogo kinyume na sheria na miongozo
iliyopo. Tunawaomba wananchi kutoa taarifa EWURA wanapoona vitendo hivyo ili
mamlaka ichukue hatua za kisheria," Amesema Musira.
Amefafanua
kuwa mbali na kuathiri ujazo halisi wa gesi, vitendo hivyo vinahatarisha maisha
ya wananchi kutokana na uwezekano wa milipuko na ajali za moto.
Musira
amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuwaeleza watoa huduma hiyo katika maduka,
kupimiwa mitungi yao kwenye mizani kabla ya kuikabidhiwa ili kuhakikisha uzito
unaendana na kiasi kilichoandikwa kwenye mtungi.
Nishati Safi ya Kupikia Yakua Tanzania
Tahadhari
hii ya EWURA inakuja wakati Serikali ikiendelea kuhamasisha matumizi ya nishati
safi ya kupikia nchini.
Kwa
mujibu wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034),
idadi ya Watanzania wanaotumia nishati safi ya kupikia imeongezeka kutoka
asilimia 1.5 mwaka 2010 hadi asilimia 6.9 mwaka 2021, ingawa kiwango hicho bado
kiko chini sana ya wastani wa dunia wa asilimia 71.
Mkakati
huo unaeleza kuwa takribani asilimia 90 ya kaya nchini bado zinategemea kuni na
mkaa kama nishati kuu ya kupikia, huku asilimia 5.1 pekee zikitumia gesi ya LPG
na asilimia 3 zikitumia umeme.
Serikali
imeweka lengo la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi
ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Matumizi ya Gesi LPG Yaongezeka
Takwimu
za Wizara ya Nishati zinaonyesha matumizi ya gesi ya LPG nchini yameongezeka
kwa kasi kutoka tani 20,000 mwaka 2010 hadi tani 160,610 mwaka 2022.
Hata
hivyo pamoja na ongezeko hilo changamoto za gharama na upatikanaji bado zinaendelea
kuwakabili watumiaji wengi. Mkakati wa Taifa unaonyesha gharama za kujaza mtungi
mdogo ni kati ya shilingi 27,000 hadi 28,000 huku bei pia ikitegemea eneo na
kampuni husika.
Kutokana
na gharama hizo watumiaji wengi
wanatarajia kupata ujazo kamili wa gesi wanayolipia. Hivyo uwepo wa
wafanyabiashara wanaodaiwa kuuza gesi yenye ujazo pungufu unaweza kuhujumu
juhudi za Serikali za kuwahamasisha wananchi kuhamia kwenye nishati safi ya kupikia.
Bei za Gesi na Soko la Ushindani
Kuhusu kupanda kwa bei za gesi, Meneja wa Mamlaka ya
Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji Kanda ya Ziwa Nyirabu Musira amesema,
EWURA haipangi bei ya gesi ya LPG moja kwa moja kwa sababu bidhaa hiyo huagizwa
kutoka nje ya nchi na kuuzwa katika mfumo wa soko huria la ushindani.
Amesema
uwepo wa kampuni nyingi zinazotoa huduma ya gesi unampa mwananchi nafasi ya
kuchagua kampuni yenye huduma bora na bei inayomfaa.
Hata
hivyo amesema mamlaka itaendelea kusimamia usalama, ubora na uhalali wa
biashara ya gesi ili kuhakikisha haki za watumiaji zinalindwa.
Kwa wananchi kama Jane na
Monica, hatua hiyo inaweza kuwa mwanzo wa kurejesha imani yao katika matumizi
ya gesi ya kupikia. Lakini kwa sasa, wanataka jambo moja tu; kila mtungi wa
gesi unaonunuliwa uwe na ujazo kamili unaolingana na fedha walizolipa.




.jpg)








