Hedhi Salama: Jinsi Ukosefu wa Taulo za Kike Unavyowanyima Wasichana wa Shule ya Msingi Kwangwa “A” Fursa ya Kushiriki Kikamilifu Katika Masomo.

0


Na Emmanuel Chibasa

Hedhi ni sehemu ya kawaida ya maisha ya mwanamke na msichana, lakini kwa maelfu ya watoto wa kike nchini Tanzania bado ni chanzo cha changamoto kinachoathiri afya, elimu, utu na ustawi wao.

Kwa baadhi ya wasichana, hedhi ni mchakato wa kibaiolojia wa kawaida, lakini kwa wengine imekuwa kikwazo kinachowafanya kukosa masomo, kupoteza kujiamini na kushindwa kushiriki kikamilifu katika maisha ya shule.

Kwa mujibu wa Wizara ya Afya Tanzania, takribani wasichana na wanawake milioni 15 kati ya watu milioni 61.7 hupitia hedhi na Ili kusimamia hedhi kwa usalama na utu, wasichana na wanawake wanahitaji upatikanaji wa taarifa sahihi, huduma za maji safi na usafi, mazingira rafiki pamoja na vifaa salama vya kujisitiri.

Katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, haki za hedhi salama zinaweza kutafsiriwa ndani ya haki za afya ya umma na haki za binadamu. Ibara ya 9(a) na (f) inaeleza kuwa mamlaka za dola na taasisi zake zinapaswa kuelekeza sera na mipango yake katika kuhakikisha utu wa binadamu na haki nyingine za msingi zinaheshimiwa na kulindwa, ikiwemo haki ya afya na elimu kwa wote.

Pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo kuboresha afya na usafi wa hedhi, changamoto bado zinaendelea kujitokeza hasa kwa watoto wa kike wanaotoka katika familia zenye kipato cha chini. Ambapo hali hii husababisha baadhi ya wanafunzi kushindwa kuhudhuria masomo wakati wa hedhi kutokana na ukosefu wa taulo za kike.

Katika Shule ya Msingi Kwangwa “A” iliyopo Kata ya Kwangwa Manispaa ya Musoma mkoani Mara, changamoto hiyo imeendelea kuwa kikwazo kikubwa kwa baadhi ya wanafunzi wa kike katika safari yao ya elimu katika shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 1, 507, Wasichana wakiwa 738  na wavulana 769 kama wanavyoeleza Lightness Jumapili,Gladness Jackson, Maria Peter pamoja na Gloria Amos.

Picha ya Wanafuzi wa Shule ya Msingi Kwangwa "A" Mara baada ya Kupatiwa Elimu ya Hedhi Salama na Kugawiwa Taulo za Kike na shirika la Rising Hope Organization

Lightness Jumapili, mwenye umri wa miaka 14, mkazi wa Mshikamano na mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Kwangwa “A”, anasema moja ya changamoto kubwa wanazokutana nazo wasichana shuleni hapo ni kukosa masomo wanapoingia katika siku zao za hedhi kutokana na kukosa taulo za kike na fedha za kununua vifaa hivyo.

Anasema wakati mwingine msichana anaweza kuingia katika siku zake akiwa shuleni bila kutarajia na kujikuta amechafuka nguo bila kuwa na nguo za kubadilisha. Hali hiyo huwasababishia aibu kubwa mbele ya wanafunzi wenzao na wakati mwingine hulazimika kuondoka shuleni kabla ya muda.

Picha kwa hisani ya Wizara ya Afya Tanzania

Kwa mujibu wa Lightness, changamoto hiyo imekuwa ikiathiri ushiriki wao darasani na kuwafanya baadhi ya wasichana kupoteza kujiamini kabisa mbele ya wenzao.

“Naiomba serikali na mashirika mbalimbali kutusaidia sisi wasichana kwa sababu sisi ndio viongozi wa baadaye. Tunahitaji kupata taulo za kike ili tuweze kuhudhuria masomo kama wanafunzi wengine,” Anasema Lightness.

Kwa upande wake Gladness Jackson mwenye umri wa miaka 12, anayesoma darasa la tano katika Shule ya Msingi Kwangwa “A”, anasema wasichana wengi wanapitia changamoto mbalimbali wanapoingia katika hedhi.

Anasema wakati mwingine mwanafunzi anaweza kuingia katika siku zake lakini akaogopa kuingia darasani au kukaa karibu na wanafunzi wengine kwa hofu ya kuchafuka na kuchekwa na wenzake na changamoto huwa kubwa zaidi pale ambapo mzazi au mlezi hana uwezo wa kununua taulo za kike.

“Msichana anaweza kumweleza mzazi kuwa ameingia katika siku zake lakini akaambiwa hakuna fedha za kununua taulo za kike. Tunaomba wazazi waelimishweshe kuhusu hedhi salama na kuhakikisha wanatusaidia kupata vifaa salama vya kujisitiri,” Anasema Gladness.

Maria Peter, mwenye umri wa miaka 12 na mwanafunzi wa darasa la sita katika Shule ya Msingi Kwangwa “A”, anasema changamoto ya kukosa taulo za kike imekuwa ikiwafanya  baadhi ya wanafunzi hukaa nyumbani kwa siku kadhaa kila mwezi kwa sababu ya kukosa vifaa vya kujisitiri, hali inayowafanya kubaki nyuma katika masomo ikilinganishwa na wenzao.

“Tunaomba serikali na mashirika binafsi waendelee kutusaidia kupata taulo za kike ili tuweze kujisitiri wakati wa hedhi na kuendelea na masomo yetu kwa sababu sisi ndio taifa la kesho,” Anasema Maria.

Naye Gloria Amos mwenye umri wa miaka 12, anayesoma darasa la sita katika shule hiyo, anasema changamoto za hedhi haziishii tu kwenye kukosa taulo za kike bali pia huathiri usalama na mustakabali wa wasichana.

Anasema baadhi ya wasichana hukumbana na vishawishi kutoka kwa vijana wa kiume wanapokosa mahitaji ya msingi hali inayoweza kuwaweka katika hatari ya mimba za utotoni na hatimaye kukatiza masomo yao.

“Wasichana wengi wanahitaji msaada wa taulo za kike ili waendelee na masomo. Tunaomba serikali na mashirika mbalimbali waendelee kutusaidia kwa sababu changamoto bado ni kubwa,” Anasema Gloria.

Kauli za wasichana hao toka shule ya msingi Kwangwa “A” zinaonyesha wazi namna hedhi inavyoweza kuwa kikwazo kikubwa kwa elimu ya mtoto wa kike pale ambapo mazingira salama na vifaa vya kujisitiri vinapokosekana.

Kulwa Gervas ni mwalimu ambaye pia ni mwalimu wa ushauri nasaha katika Shule ya Msingi Kwangwa “A”, anasema changamoto ya wanafunzi wa kike kushindwa kuhudhuria masomo wakati wa hedhi bado ni kubwa kutokana na hali za kiuchumi za baadhi ya familia na mara nyingi wanafunzi hukosa kueleza sababu halisi za kutokuwepo shuleni kwa hofu au aibu.

“Wakati mwingine mwanafunzi anarudi shule baada ya siku kadhaa na ukimuuliza anakueleza kuwa alikuwa kwenye siku zake lakini hakupata taulo za kike. Wengine huambiwa kutumia vitambaa vya kawaida ambavyo muda mwingine sio salama.

Tunaiomba serikali na wadau kuongeza uwekezaji katika shule za msingi sababu tunaona nguvu kubwa inaelekezwa katika shule za Sekondari, huku katika shule za msingi changamoto ni kubwa kuliko inavyofikiriwa,” Anasema Kulwa.

Kulwa anaongeza kuwa watoto wanaanza kubalehe katika umri mdogo zaidi kuliko zamani  hali inayokdiriliwa kuwa zaidi aslimia hamsini ya wasichana hukosa masomo  katika shule hiyo kutokana na changamoto ya hedhi jambo linaloongeza uhitaji wa msaada wa taulo za kike na elimu ya hedhi salama zaidi katika shule za msingi.

Rose Nyamhanga ni mama wa watoto watatu mkazi wa Mwisenge manispaa ya Musoma mzazi wa mmoja wa wanafunzi wa Shule ya anasema changamoto ya kipato imekuwa ikiwafanya baadhi ya wazazi kushindwa kumudu gharama za kununua taulo za kike kila mwezi.

“Tunawashukuru wadau wanaotusaidia kwa sababu kuna wazazi ambao hawawezi kumudu gharama hizi kila mwezi. Msaada huu unawasaidia watoto wetu kuendelea na masomo,”

Changamoto ya hedhi salama inayowakabili wasichana wa Kwangwa inaakisi hali inayoshuhudiwa sehemu mbalimbali nchini.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Hedhi Salama Duniani yaliyofanyika wilayani Kibondo mkoani Kigoma, Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, kwa niaba ya Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa, alitoa wito kwa jamii, taasisi za umma na binafsi kushirikiana kuondoa unyanyapaa wa hedhi na kuhakikisha huduma rafiki za hedhi salama zinapatikana kwa wanawake na wasichana ili kuwawezesha kuishi kwa utu, usalama na heshima.

Dkt. Samizi alisema hedhi ni mabadiliko ya kawaida ya kibayolojia na si ugonjwa wala jambo la kuaibisha, hivyo jamii inapaswa kuondoa mila potofu na unyanyapaa unaowakwamisha wasichana kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kielimu.

Alieleza kuwa tafiti zinaonesha asilimia 27 ya wasichana nchini hukosa shule angalau siku tatu kila mwezi kutokana na changamoto za hedhi, jambo linalowapotezea zaidi ya siku 30 za masomo kwa mwaka na kuathiri maendeleo yao kitaaluma.

Kwa mujibu wa Dkt. Samizi, Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha miundombinu rafiki ya hedhi salama ikiwemo ujenzi wa vyoo bora vyenye huduma ya maji, usafi na mazingira salama ya kujifunzia mashuleni ili kulinda afya, utu na heshima ya wanawake na watoto wa kike nchini.

Bakari Nyamsosa ni Mkurugenzi wa shirika la Rising Hope Organization Tanzania lenye makao yake makuu Manispaa ya Musoma Mkoani Mara, Akizungumza na Musoma Tv mara baada ya kutoa msaada na kugawa taulo za kike kwa wanafunzi wa shule ya msingi Kwangwa “A” anasema shirika hilo lilianza programu ya kugawa taulo za kike baada ya kubaini idadi kubwa ya wasichana kukosa masomo katikati na mwishoni mwa mwezi.

Anasema utafiti wao ulibaini kuwa sababu kubwa ilikuwa ni ukosefu wa taulo za kike, jambo lililosababisha wasichana kukosa shule kwa siku nne hadi tano kila mwezi.

Kutokana na hali hiyo, Rising Hope Organization ilianza kugawa taulo za kike mashuleni ili kuongeza mahudhurio na kuimarisha kujiamini kwa wasichana.

Picha ya Mkurugenzi wa Rising Hope Organization Bakari Nyamsosa Akikabidhi Msaada wa Taulo za Kike kwa Mwalimu Kulwa Gervas wa Shule ya Msingi Kwangwa "A"

“Baada ya kuanza kutoa taulo za kike tumeshuhudia ongezeko la mahudhurio ya wasichana shuleni. Lakini mahitaji bado ni makubwa kuliko uwezo wetu. Tunahitaji ushirikiano wa serikali na wadau ili kuwafikia wasichana wengi zaidi,” Amesema Bakari.

Picha: Bakari Nyamsosa, Mkurugenzi wa Rising Hope Organization na Mwalimu wa Ushauri Nasaha Kulwa Gervas Wakigawa Taulo za Kike wa Wanafunzi wa Darasa la Sita Shule ya Msingi Kwangwa 

Kwa mujibu wa Wizara ya Afya Tanzania hedhi isiyo salama inaweza kusababisha maambukizi ya njia ya mkojo (UTI), magonjwa ya mfumo wa uzazi na kuathiri maendeleo ya mwanamke kielimu, kijamii na kiuchumi.

Wizara ya Afya inahimiza jamii kuwasaidia wasichana kumudu hedhi kwa njia salama na yenye utu, huku wazazi, walimu na jamii wakihimizwa kutoa elimu sahihi kuhusu hedhi na balehe.

Kila mwaka Mei 28 huadhimishwa Siku ya Hedhi Salama Duniani kwa lengo la kuongeza uelewa, kupinga unyanyapaa na kuhamasisha upatikanaji wa huduma rafiki za hedhi kwa wasichana na wanawake.

Kaulimbiu ya mwaka 2026 ni: “Wezesha Mazingira ya Hedhi Salama yenye Utu kwa Wasichana na Wanawake Wote.”

Picha kwa hisani ya Wizara ya Afya Tanzania

Kwa wasichana wa Kwangwa, kaulimbiu hiyo si maneno tu bali ni matumaini ya siku zijazo ambapo hakuna mtoto wa kike atakayelazimika kukosa masomo, kupoteza kujiamini au kuacha ndoto zake kwa sababu ya kukosa taulo za kike.







 

Chapisha Maoni

0 Maoni
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Chapisha Maoni (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top