Zaidi ya Shilingi Milioni 624.6 Zarejeshwa na TAKUKURU Kagera

0


 Na Angela Sebastian 

Bukoba: Taasisi ya kuzuia  na kupambana  na rushwa (TAKUKURU) Mkoani Kagera  imefanikisha kurejesha zaidi ya shilingi milioni 624.6 baada ya  kushinda kesi 50 kati ya 52 zilizoendeshwa  katika mahakama mbalimbali za mkoa wa kagera kwa kipindi cha Julai 2025 hadi sasa.

Akitoa taarifa ya kipindi cha  kuanzi Januari hadi Machi mwaka huu kwa waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari mjini Bukoba,Naibu mkuu wa Takukuru  mkoani humo  Leonard Swai ameeleza kuwa,kwa kipindi  cha Julai 2025 hadi sasa walifanikiwa kufungua kesi 61 mahakamani ambapo mashauri 52 yameamuliwa  kati ya hayo takukuru imeshinda mashauri 50 sawa na asilimia 97 ,imeshindwa mashauri mawili na mashauri 9 yanaendelea mahakamani.

Amesema katika mashauri 50 ambayo Takukuru imeshinda wamefanikiwa kurejesha kiasi cha zaidi ya shilingi  milioni 624.6  ambapo kwa Januari  hadi Machi  2026 wamepokea taarifa 132  kati ya hizo 83  zilihusu rushwa na taarifa 49 hazikuhusu rushwa.

Alieleza kuwa Takukuru wilaya ya  Kyerwa imefanikiwa kurejesha fedha kiasi cha shilingi milioni 30  zilizotolewa kwa ajili ya mkopo wa kikundi cha ufugaji nyuki cha wanawake  wa Kata ya Katera  ambazo ni asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri.

Alisema kikundi hicho kilipokea fedha kupitia akaunti ya kikundi namba 35910010751 iliyopo benki ya NMB tarehe 18.Februari mwaka huu baada ya kuonekana kutimiza masharti yote ya mkopo.

Alisema baada ya uchunguzi wa Takukuru  ilibaini kuwa kikundi hicho kimetumika kama kikundi kivuli  cha kupata mkopo husika wa milioni 30 baada ya kikundi hicho kivuli kuwekewa milioni 30 kisha  zilihamishiwa kwenye akaunti namba 01J2033984900 inayomilikiwa na Benjamin Barthazari ambaye alizitumia fedha hizo kwa matumizi yake binafsi.

Alisema baada ya kubaini kasoro hizo Takukuru Kyerwa  ilielekeza fedha hizo zirejeshwe kwenye halmashauri ya Kyerwa ili zitumike kama ilivyokusudiwa kwa kikundi cha wanawake .

Aidha Takukuru wamefanikiwa  kudhibiti ujenzi wa chini  ya kiwango  wa  msingi wa jengo la Zahanati  ya Kijiji cha Runzenze Kata Ntobeye Wilayani Ngara  inayojengwa kwa nguvu za wananchi na jumla ya shilingi milioni 9.5 kimekusanywa na  wananchi  wa kijiji hicho kwaajili ya ujenzi wa zahanati hiyo.

Alisema ufuatiliaji huo ulibaini  kuwa kiwango cha uwiano  katika  mchanganyiko wa zege ( concrete ratio ) katika jamvi la msingi  huo kuwa ni dhaifu kiasi cha kusababisha jamvi kuanza  kumomonyoka na Nondo zilizosukwa kuonekana na kuanza kupata kutu hali inayoashiria ujenzi umefanyika chini ya kiwango.

Takukuru kwa kushirikiana na ofisi ya mkurugenzi wa Halmashauri, waliishauri Serikali ya Kijiji kufanya marekebisho katika hatua hiyo ya ujenzi ili kuuia madhara ambayo yangejitokeza kutokana na udhaibu wa msingi huo jamba ambalo limekwisha tekelezwa.

Alisema pia kwa kipindi cha Januari hadi Machi mwaka huu taarifa 83  zilizohusu  rushwa zilichunguzwa  na jumla ya majalada 12 yalifunguliwa kesi mahakamani na chunguzi  zinaendelea.






Chapisha Maoni

0 Maoni
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Chapisha Maoni (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top