Na Mwandishi Wetu, Musoma.
KATIKA kupambana na vitendo vya ukatili wa Kijinsia, Wasichana 4,481 waliokuwa katika hatari ya kukeketwa na familia zao mkoani Mara wameokolewa kuanzia mwaka 2017 hadi 2025.
Hayo yamebainishwa hivi karibuni na Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la 'Hope for Girls and Women in Tanzania' (HGWT) Rhobi Samwelly, linalopambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia mkoani humo alipokuwa akizungumza na Musoma News Hub.
Amesema kuwa ushirikiano kati ya serikali Mkoani humo, shirika hilo na wananchi umewezesha kuwaokoa wasichana hao na kuwapatia hifadhi katika nyumba salama zinazomilikiwa na kuendeshwa na shirika hilo. Huku wengi wao ni kutoka Wilaya za Tarime na Serengeti.
“Kwa kipindi hicho tulikuwa tukiwaokoa na kuwahifadhi katika vituo vya Butiama nyumba Salama na Hope Mugumu. Wakiwa huko hupata huduma mbalimbali kama msaada wa kisaikolojia, huduma za afya, mahitaji muhimu, elimu, msaada wa kisheria na huduma za kiroho,” alisema Rhobi.
Ameongeza kuwa, baadhi ya wasichana hao wamefanikiwa kielimu baada ya kusaidiwa na shirika hilo, ambapo wamehitimu katika vyuo vikuu, vyuo vya kati na vya ufundi. Ambapo Kwa sasa, baadhi yao wamejiajiri huku wengine wakiwa wameajiriwa na hivyo, kusaidia familia zao na jamii kwa ujumla.
Aidha, Rhobi amesema amesema kuwa, Shirika hilo litaendelea kushirikiana na serikali, wadau mbalimbali pamoja na Wananchi ikiwemo Kutoa elimu ya ukatili kwa Jamii katika kuhakikisha kwamba ustawi bora unaimarika kwa ajili ya maendeleo.


