Mwandishi Wetu, Musoma.
Imebainishwa kuwa, jukumu la kuhakikisha usalama wa watoto si la mtu mmoja, bali ni dhamana ya kila mtu kushiriki kikamilifu kuona kwamba, watoto wanalelewa katika mazingira salama na bora.
Akizungumza na Musoma News Hub, Mkurugenzi wa Shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania linalopambana na ukatili Mkoa wa Mara, Rhobi Samwelly, amesema watoto ni hazina ya taifa inayohitaji ulinzi wa pamoja. Huku akisema kila mwana Jamii atambue wanapaswa kuishi bila hofu ili waweze kukua na kutimiza ndoto zao.
Rhobi amesema vitendo vya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji huacha majeraha ya kudumu kwa watoto. Ameonya kuwa, kimya cha jamii huwapa nguvu wanaofanya ukatili kuendelea na vitendo vyao, hivyo akasisitiza umuhimu wa kuripoti matukio ya ukatili Katika vyombo vya sheria.
Aidha, amesema vyombo vya habari na mashirika yasiyo ya kiserikali mchango wao ni mkubwa katika kuhamasisha jamii kushiriki katika mapambano ya ukatili wa Kijinsia. Ambapo ameomba ushirikiano uendelee kuwepo kati ya serikali, taasisi mbalimbali na wananchi katika kusaidia usalama wa watoto kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


