Mila ya Ukeketaji Kikwazo cha Haki na Ndoto za Wasichana

0


Sehemu ya Pili


Na Emmanuel Chibasa

Katika makala ya awali tulishuhudia simulizi za huzuni na matumaini ya wasichana wa Kikurya waliokimbia ukeketaji na ndoa za utotoni ili kulinda ndoto zao, Hata hivyo simulizi hizo hazijaishia kwao pekee, kwani tatizo la mila kandamizi bado linaendelea kuathiri jamii na wadau wa maendeleo.

Licha ya juhudi za serikali na wadau mbalimbali bado kunahitajika elimu ya kina ili kubadirisha fikra kwa jamii juu ya mila zinazonyima wasichana haki ya kusoma, kuamua mustakabali wao na kuishi maisha yenye utu.

Wakati vitendo vya ukatili vikitajwa kupungua katika baadhi ya maeneo nchini, wataalamu na wadau wa maendeleo wanashauri kuwa, bado mabadiliko ya kimila yanahitaji muda mrefu kufikiwa, Wakieleza kwamba, mila na desturi zimejengeka kwa vizazi vingi, na mara nyingine huchukuliwa kama chanzo cha heshima au utambulisho wa kijamii.

Waziri wa maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt Dorothy Gwajima mwaka 2025 alitangaza kushuka kwa matukio ya ukatili dhidi ya watoto na vijana ikilinganishwa na utafiti uliofanyika mwaka 2009.

Akitangaza Matokeo ya utafiti wa kitaifa wa ukatili dhidi ya watoto na Vijana ya mwaka 2024 tarehe 9 June 10, 2025 Mhe. Gwajima alisema, Matokeo ya utafiti wa Machi-Juni, 2024 yanaonesha ukatili umeshuka kwa kiwango kikubwa ukilinganisha utafiti wa 2009 ambapo, kwa watoto wa kike: Ukatili wa kingono umepungua kutoka 33% hadi 11%; Ukatili wa kimwili umepungua kutoka 76% hadi 24%; na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka 25% hadi 22%.

Kwa watoto wa Kiume: Ukatili wa kingono umepungua kutoka 21% hadi 5%; Ukatili wa kimwili umepungua kutoka 74% hadi 21% na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka 31% hadi 16%.

Licha ya matokeo hayo kuonesha kushuka kwa viwango vya ukatili dhidi ya watoto na vijana, wadau wa maendeleo wanasema bado changamoto kubwa katika utekelezaji wa sheria na mabadiliko ya kijamii.

Nollasko Mgimba ni Afisa Miradi kutoka Kanisa Katoliki Jimbo la Musoma, anasema kupungua ni ishara nzuri ya mafanikio lakini hakumaanishi tatizo limekwisha, kwani changamoto ya utekelezaji wa sheria, mitazamo ya jamii na hofu ya viongozi kupoteza nafasi zao za uongozi bado inakwamisha mapambano ya kutokomeza ukatili.

                Picha Nollasko Mgimba Afisa Miradi Kanisa Katoriki Jimbo la Musoma

Mgimba anasema changamoto kubwa wanayokutana nayo kama wadau wa maendeleo ni kutokukubalika kirahisi katika jamii, kwani mara nyingi watendaji wa mashirika ya kupinga ukatili huonekana kama wapinzani wa mila na desturi ambazo jamii huzichukulia kuwa vyanzo vya heshima na hata kipato. Hali hii husababisha baadhi ya wanajamii kushikilia mila hizo kwa nguvu na kutotoa ushirikiano katika jitihada za kutokomeza vitendo vya ukatili.

“Tunayo changamoto  kwenye usimamizi wa sheria na sera zilizopo, kwa sababu jambo hili ni la kimila, unakuta katika maeneo haya kuna viongozi wengi wanaochaguliwa au kuteuliwa wanaotoka katika mazingira haya, Katika mapambano haya wanakosa nguvu kubwa ya kusimamia sheria na sera zilizopo kutokana na wao kuwa sehemu ya mila na desturi hizo na wanahofia kupoteza nafasi zao za uongozi kwa kuchaguliwa au kuteuliwa ” Amesema Mgimba.

SMAUJATA ni kampeni ya kitaifa ya kupinga ukatili wa kijinsia na ukatili kwa watoto nchini Tanzania inanyofanya kazi chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii , Jinsia, Wanawake na Watoto na Mkundi maalum. Joyce James ni Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa wa Mara, anasema bado kunahitajika elimu ya kina katika jamii kuhusu madhara ya mila ya ukeketaji na ndoa za utotoni ili kuondoa imani potofu zinazowalazimisha wasichana kuingia katika ndoa au kukeketwa bila ridhaa yao.

                        Picha: Joyce James Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa wa Mara

“Bado jamii inapaswa kupewa elimu zaidi kufahamu madhara ya ukeketaji na ndoa za utotoni, mfano unakuta msichana analazimishwa kukeketwa au kuolewa bila ridhaa yake wasichana hawa ukumbana na madhara mengi, wananyanyasika, wanakutana na vitendo vya kikatili sasa msichana kama huyu hawezi kufurahia maisha ya ndoa na hapa ndio tunatengeneza kizazi cha ma single mother wengi katika jamii yetu” Amesema Joyce

Naye Neema Ndoboka kaimu mkurugenzi idara ya maendeleo ya jamii akizungumza wakati akifungua kikao cha wadau wanaotekeleza eneo la mila na desturi katika Mpango wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (MTAKKUWA) Septemba 17,2025 mkoani Dodoma, amesema serikali inaendelea na juhudi za kuchochea maendeleo katika jamii kupitia afua mbalimbali ikiwemo utoaji wa elimu juu ya masuala ya mila na desturi zisizofaa  kupitia mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na kushirikiana na wadau wa maendeleo.

Amesema serikali inatambua na kuthamini mchango wa wadau wa maendeleo katika kuleta na kupambana zaidi katika kutoa elimu kwa jamii ili kufikia malengo ya mabadiriko  katika jamii, lakini suala la mila na desturi linachukua muda hivyo wanapaswa kutokata tamaa.

Baada ya kufanya mahojiano na wadau hao wa maendeleo nilibaki na maswali ya kujiuliza je, dini inasemaje kuhusu  ukeketaji na ndoa za utotoni na kama mila na ndoa hizi za utotoni zinatambulika kidini?

Nimezungumza na Sheikh Omari Ali Hamisi kutoka Masid Musoma, anasema katika jamii kuna muingiliano wa mila ikiwa ni pamoja na mila ya ukeketaji ambayo madhara yake ni makubwa kuliko faida na kupelekea pia wasichana chini ya umri wa miaka 18 kuingia katika ndoa za utotoni.

Amesema ndoa kwa mujibu wa dini ya kiislamu na kwa mujibu wa sheria za dini , ndoa ni ibada na mtu anapoingia kwenye ndoa ameingia kwenye taasisi ya ibada na inaongozwa kwa kanuni zake.

       Picha: Sheikh Omari Ali Hamisi kutoka Masid Musoma

“Tunapozungumzia ndoa za utotoni, tunazungumzia ndoa ambazo ziko chini ya ule umri ambao unatambulika kisheria ima kitamaduni, au sheria ya nchi au kwa madhehebu na imani tofauti tofauti.

Ili kutokomeza tatizo hili kwanza inapaswa kutolewa elimu baina ya mtu na mtu, familia, kitongoji, kijiji na maeneo mbalimbali katika jamii kuelimishana madhara yanayopatikana kuhusiana ukeketaji madhara ya kiafya, kisaikolojia na kiuchumi yanayopatikana kutokana na ukeketaji na ukatili wa kijinsia kwa wasichana na watoto.

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top