Mila ya Ukeketaji Kikwazo cha Haki na Ndoto za Wasichana

0


 



Sehemu ya Kwanza


Na Emmanuel Chibasa

Kila binti wa Kikurya anayekanyaga darasa la kwanza hubeba ndani yake ndoto kubwa ndoto ya maisha yake ya baadae, lakini nyuma ya tabasamu na matarajio hayo, wingu zito la mila ya ukeketaji hujificha, likisubiri kuzima ndoto hizo kwa kisingizio cha heshima na maandalizi ya ndoa za utotoni.

Mara nyingine binti analazimishwa kuchagua kati ya elimu na ndoa, ama kati ya maisha ya ndoto yake na mateso ya kimila. Nikukaribishe katika simulizi ya matumaini na majonzi, inayoonesha namna haki na ndoto za wasichana zinavyopigwa vita katika jamii ya Kikurya kabila kubwa linalopatikana nchini Tanzania, Kenya na Uganda.

Ni majira ya saa kumi na mbili jioni nafika katika kijiji cha nyamisisi kiabakari wilaya ya Butiama mkoani Mara Tanzania, na kutana na Veronica Ryoba (sio jina lake halisi) msichana mwenye umri wa mika 18 sasa ambaye ni miongoni mwa wasichana  waliokimbia familia zao kutokana na kulazimishwa kuolewa.

Veronika anasema alilazimika kukimbia familia yake na kwenda kwa baba yake mdogo ambaye alimsomesha hadi darasa la 7 na baadae kutafuta hifadhi katika kituo cha nyumba salama cha Hope for Girls and Women Tanzania kilichopo wilaya ya Butiama mkoani Mara Tanzania.

Picha ya Veronica Ryoba Akiwa katika Kituo cha Hope For Girls and Women Tanzania Butiama mkoani Mara

Anasema mwaka 2020 akiwa na umri wa miaka 13 baba yake mzazi alimlazimisha kukeketwa ili aweze kuolewa, na familia yao ipate  mahari ambayo ingemsaidia mdogo wake wa kiume, ambaye naye alikuwa anashawishiwa kuacha masomo ili aweze kutumia mahari hiyo kuoa. Jambo ambalo mama yao alilipinga vikali.

Veronika anaeleza kuwa siku moja baba yao alirudi nyumbani akiwa amelewa na alikuta mama yao hajamuachia chakula, hali iliyosababisha ugomvi mkubwa hali iliyoplekea baba yao kuchukua panga na kumkamkata na kumsababishia kifo mama yao.

Kutokana na huzuni ya kupoteza mtetezi baada ya kumalizika kwa mazishi ya mama yao, Veronika aliamua kutoroka kwani baba yao aliendelea kumlazimisha kukeketwa ili aolewe.

“Mwaka 2020 nilikimbia ukeketaji kwa sababu baba yangu alikuaga mlevi sana na alikua anataka mimi nikeketwe ili niolewe apate mahari  imsaidie mdogo wangu wa kiume kuoa na kuendelea na maisha yake.

Nilipotoroka nilifika hapa nyumba salama nikapokelewa vizuri  na nikawaeleza changamoto nilizopitia kule kijijini, wakanisaidia na nikafanikiwa  kuanzia kidato cha kwanza hadi nikafanikiwa kuhitimu mwaka 2024 kidato cha nne shule ya sekondari Kyabakari, nimefaulu vizuri  na nategemea kuendelea na masomo yangu.” Anasema Veronica

Ameongeza kuwa ukatili aliofanyiwa umeathiri pakubwa maisha yake kwanza kama mzazi wake angefanikiwa kumkeketa asiwengeza kufikia malengo yake ya kumaliza elimu ya msingi na sekondari.

Mbali na Veronica, Lucia Wambura ambaye pia sio jina lake halisi, naye amekumbana na changamoto ya kulazimishwa kukeketwa na ndugu wa baba yake ili aweze kuolewa mara tu baada ya kumaliza elimu yake ya msingi.

Lucia anasema tangu akiwa mdogo, baba yake alikua anampenda sana na katika familia yao wazazi wake alisikia wakipinga mila ya ukeketaji huku akiwasihi watoto wake ikiwa ni pamoja na dada zake wasome kwa bidii, waweze kufaulu vizuri katika masomo yao na sio kukeketwa ili waolewe.

Picha ya Lucia Wambura Akiwa katika Kituo cha Hope For Girls and Women Tanzania Butiama mkoani Mara

Anasema mara baada ya baba yake mzazi kufariki mwaka 2020, alishangaa kuona ndugu upande wa baba yake wakibadilika na kuonesha dalili za kuanza taratibu za kutaka akeketwe mara baada ya kumaliza mtihani wa darasa la saba.

“ Kwa bahati mbaya  baba yangu alifariki mwaka 2020 nikiwa darasa la tatu, na baada ya hapo nilianza kufuatiliwa na ndugu upande wa baba walitaka nikakeketwe. Yaani nilikua naandaliwa kukeketwa baada ya kumaliza mtihani wa darasa la saba nilipogundua hila yao nilitoroka nyumbani na kukimbilia kwa rafiki yangu ambaye tumemaliza nae darasa la saba, ambapo mama yake alinipeleka dawati ambao walinileta hapa nyumba salama ”

Lucia anasema ni ngumu kwake kuishi mbali na familia yake kwani hakuwahi kudhani kuna siku ataishi mbali na familia yake lakini kwa sasa imetokea na anaishi  nyumba salama na mabinti wenzake.  

“Kuondoka nyumbani pia kuliathiri masomo yangu maana muda mwingine nikiwa nasoma nawaza  nyumbani nakumbuka familia yangu na ndugu zangu wengine niliowaacha kule nyumbani”

Nashauri jamii inayoendeleza mila ya ukeketaji iachane nayo, kwa sababu inatuathiri sisi mabinti kisaikolojia, na pia waachane imani potofu kuwa binti asiyekeketwa hawezi kuolewa na mwanaume wa kikurya.” Amesema Lucia.

Kwa miaka kadhaa mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na wadau wengine wa maendeleo, yamekua yakishirikiana na serikali katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia hususani ukeketaji, ndoa za utotoni na athari zake kiafya  kwa kutoa elimu pamoja na kutoa msaada kwa wasichana wanaokimbia familia zao kutokana na kulazimishwa kukeketwa.

Ripoti ya utafiti ya afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria Tanzania ya mwaka 2022, Inaonesha kuwa Mkoa wa Mara ni miongoni mwa mikoa mitano hapa nchini, inayoongoza kwa mimba za utotoni ambapo mkoa wa Songwe ndio unaongoza kwa kuwa na asilimia 45%, ukifuatiwa na mkoa wa Ruvuma wenye asilimia 37% Katavi ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na asilimia 34%, Mkoa wa Mara ukishika nafasi ya nne ukiwa na asilimi 31% na mkoa wa Rukwa ukishika nafasi ya Tano ukiwa na asilimia 30%

Katika Ripoti ya utafiti ya mwaka 2024 pia inaonesha mkoa wa Mara unashika nafasi ya tatu kwa matukio ya ukatili wa kijinsia kwa kuwa na asilimia 28, huku mikoa ya Arusha na Manyara ikiwa vinara wa matukio ya ukatili wa kijinsia kwa kuwa na asilimia 43%

Hali hii inadaiwa kuchangiwa mila na desturi kandamizi kama jambo la heshima na utambulisho wa ulinzi na ujasiri kwa mwanamke lakini kwa undani wake, ni mfumo unaonyima wasichana haki ya kufanya maamuzi kuhusu miili yao na maisha yao ya baadaye.  

Visa kama hivi vinawapata wasichana walio wengi ambao wanakumbana na changamoto kama hizi, lakini wanakosa fursa ya kupaza sauti zao ili jamii iweze kuona jinsi mila hii inavyowathiri  maisha yao na kushindwa kutimiza ndoto zao.

 Rhobi Samwelly ni mkurugenzi wa wa shirika la Hope for Girls and Women Tanzania lilioanzishwa kwa lengo la kupinga na kuondoa ukatili katika jamii ambao pia kupitia mradi wa nyumba salama zilizopo wilaya ya Butiama na Serengeti mkoani Mara, kwa ajili ya kuhifadhi wasichana wanaokimbia vitendo vya ukatili, anasema jamii inawaona kama wasaliti  wanapo wasaidia wanawake na mabinti wanaofanyiwa vitendo vya ukatili.

“ Wakati mwingine tunapotekeleza majukumu yetu tunatukana  changamoto ya watu kutukatisha tamaa, lakini sisi tuandeleza mapambano ili kuhakikisha hili kundi linapata haki na kutimiza ndoto zao na pia kuhamasisha vijana wa kiume kusoma kwa bidii ili na wao watengeneze maisha yao Tunabadilisha mitazamo kwa vijana wa kiume kuwa wasiishi kwa kuwategemea dada au wadogo zao wa kike kama vitega uchumi cha wao kupata mahali ”

Rhobi Samwelly Mkurugenzi wa Shirika la Hope for Girls and Women Tanzania

Rhobi ameongeza kuwa Jamii bado inahitaji elimu sana kuhusu madhara ya vitendo hivi vya ukatili maana mabadiliko katika mila na desturi yanakuja taratibu, na kuwataka wanahabari kuendelea kuibua visa na simulizi ambazo hazizungumzwi katika jamii zetu ili wengine wapate kujifunza.

             Itaendelea Sehemu ya Pili..

                                                                               

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top