Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Prof. Peter L. M. Msoffe amewataka wadau wanaojishughulisha na maendeleo ya zao la mpunga kufanya kazi kwa ubunifu na bidii kubwa hatua itakayosaidia kuyashika masoko ya nje ya nchi na kukuza maendeleo nchini.
Amesema hayo tarehe 3 Juni 2026, jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa Wadau wa Mpunga waliokutana kujadiliana mkakati wa maendeleo ya uzalishaji wa zao hilo ambalo uendelezwaji wake unafadhiliwa na Serikali ya Japan kupitia Shirika la Kimataifa la Ushirikiano la Japan (JICA).
Naibu Katibu Mkuu Prof. Msoffe mbali na kupongeza jitihada zinazofanywa na JICA katika kuendeleza zao la Mpunga na kueleza kuwa ni baada ya miaka mingi ya ushirikiano na Serikali ya Japan kupitia JICA mabadiliko makubwa yamepatikana katika Sekta ya Kilimo, hususan katika zao la mpunga hivyo ni muda wa kuhakikisha msukumo unawekwa ili miaka mingi ijayo kuwe na maendeleo makubwa.
Akizungumzia mafanikio ya zao la Mpunga, Prof. Msoffe amebainisha kuwa Mpunga ni kati ya mazao ya kimkakati hapa nchini linalotoa mchango mkubwa kwenye suala zima la uhakika wa chakula huku likitumiwa na wananchi wengi, ikilinganishwa na zamani ambapo lilikuwa ni zao la kuliwa kama chakula kwenye shughuli maalumu kama sikukuu au sherehe.
Katika mkutano huo, wadau wa Mpunga pia walitumia nafasi ya kumuaga Bw. Kenji Shiraishi ambaye kwa miaka mingi kupitia JICA amekuwa akiratibu uendelezwaji wa zao la Mounga nchini. Kwa sasa amehamishiwa nchini Uganda kuendeleza zao la Mpunga ambapo katika hotuba yake ya kuaga alipongeza ushirikiano mzuri na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza zao la Mpunga nchini.
✍️wizara ya kilimo


