Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na IUCN wameandaa na kuratibu warsha ya siku tatu kuhusu Usimamizi wa Mazingira na Udhibiti wa Taka za Plastiki katika Maeneo ya Ukanda wa Pwani na Bahari. Warsha hii imeanza rasmi tarehe 2 Machi 2026 mkoani Morogoro. Warsha hii ni pamoja na kupata taarifa ya mradi wa “Pamoja Tuhifadhi Bahari Yetu” unaoratibiwa na IUCN. Ufunguzi wa warsha hiyo umefanywa na Dkt. Rose Sallema Mtui kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Dkt. Rose Sallema alisisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kushirikiana katika kubadilishana uzoefu na kutafuta suluhisho la pamoja kuhusu changamoto za utunzaji wa mazingira, hususan katika udhibiti wa taka ngumu. Aidha, alieleza kuwa warsha hiyo inalenga kujadili na kubaini mikakati ya kudhibiti taka za plastiki kwenye maeneo ya pwani na baharini ili kulinda rasilimali za mazingira kwa manufaa ya jamii.
Dkt. Rose aliwashukuru wadau wa IUCN kwa kufadhili warsha hiyo na kuunga mkono juhudi za NEMC katika kutekeleza majukumu yake ya kulinda mazingira. Pia aliahidi kuwa NEMC itaendelea kutoa ushirikiano na msaada unaohitajika kuhakikisha malengo ya mradi yanafikiwa kikamilifu na kwa mafanikio makubwa.
✍️nemc











