Na Jackline Minja - WMJJWM
Misungwi: Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amewataka wananchi wa Kijiji cha Koromije wilayani Misungwi mkoani MwNza na watanzania wote kwa ujumla kuhamasika na kujenga nyumba bora katika maeneo yao ili kuboresha afya na Ustawi wao.
Naibu Waziri Mahundi ameyasema hayo wakati wa ziara yake katika Wilaya Misungwi iliyolenga kuangalia namna wananchi wanavyohamasika katika ujenzi wa Makazi Bora aliyoifanya Desemba 23, 2025.
Akizungumza na wanakikundi wanaohamsishana kwa kujengeana nyumba kijijini hapo, Naibu Waziri Mahundi amewapongeza wanakikundi kwa jitihada zao za kujengeana nyumba bora na kuhimiza Maafisa Maendeleo ya Jamii kuendelea kuhamasisha jamii kuona umuhimu wa kuwa na nyumba bora.
Aidha Naibu Waziri Mahundi ameshiriki kujenga nyumba iliyopo katika hatua ya msingi ikiwa ni kuhamasisha wananchi kuongeza ari ya kushiriki kwa hiari katika miradi ya maendeleo na kuboresha makazi yao huku akiunga mkono jitihada za wananchi kwa kuwachangia mifuko 15 ya saruji, hatua iliyochochea mshikamano na ari ya kushirikiana katika eneo hilo.
“Kampeni ya Makazi Bora si tu ya kujenga nyumba bali pia ni fursa ya kukuza moyo wa mshikamano, kusaidiana na kujenga jamii yenye maendeleo endelevu. Wizara inategemea ushirikiano wa wananchi, kujitolea kwa hiari na kushirikiana kwa dhati katika miradi hii ya Makazi bora ambayo ni msingi wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.” amesema Naibu Waziri Mahundi
Akizungumza kwa niaba ya wanakikundi cha BAPONYWAMASWA Katibu wa Kikundi hicho Joyce Lupemba amesema ushirikiano wa wananchi na wadau wa maendeleo ni kiini cha kufanikisha miradi ya makazi bora kwa gharama nafuu, jitihada hizi zinawawezesha kuishi katika makazi salama, yenye hadhi, na zinazozalisha mshikamano wa kijamii kama ilivyokuwa katika mila za kiasili za kuchangiana nguvu kazi.
Chanxo: maendeleo ya jamii












