Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limezitaka taasisi za umma zikiwemo Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 na Kanuni zake yanatekelezwa ipasavyo katika maeneo yao ya kazi.
Wito huo umetolewa leo, tarehe 20 Agosti 2025, katika semina ya mafunzo ya nyenzo za usimamizi wa mazingira chini ya Mradi wa EMA kwa Taasisi za Umma inayoendelea katika Hoteli ya Midland, Jijini Dodoma kuanzia tarehe 20 hadi 21 Agosti 2025.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, mgeni rasmi ambaye ni Meneja wa Maeneo Maalumu na Mabadiliko ya Tabianchi, Dkt. Careen Anatory Kahangwa, amesema lengo la semina hiyo ni kuimarisha mbinu za kazi na uwezo wa utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, sambamba na kuimarisha mifumo ya kisheria na kitaasisi kwa ajili ya usimamizi bora wa mazingira nchini.
"Ushiriki wenu katika kikao hiki ni wa muhimu kwa kuwa unalenga kuhakikisha utekelezaji wa sheria za kitaifa na mikataba ya kimataifa ya mazingira. Hii itawezekana tu iwapo mtayapokea mafunzo haya kwa umakini na kuyazingatia ili kujengewa uwezo wa kutosha katika kusimamia vyema mazingira," alisema Dkt. Kahangwa.
Kwa upande wake, Afisa Mazingira Mkuu wa NEMC na Mratibu Mkuu wa Mradi wa EMA, Bw. Paul Mashaija Kalokola ameeleza kuwa kumekuwa na uhitaji mkubwa wa kujengea uwezo taasisi mbalimbali ili wadau waweze kufahamu na kutumia nyenzo muhimu za usimamizi wa mazingira nchini.
Ameongeza kuwa changamoto kubwa kwa sasa ni udhaifu wa baadhi ya taasisi katika kutekeleza ipasavyo Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa mradi huo wa miaka mitatu unaosimamiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais, wenye lengo la kuimarisha uwezo wa wadau wote nchini katika kusimamia mazingira kwa ufanisi.
@nemc Tanzania