Binti ni Mtoto Sio Mke: Simulizi Za Wasichana Waliokimbia Ndoa Za Utotoni Mara

0




Na Emmanuel Chibasa

Binti ni mtoto Sio mke, hii ni kauli mbiu ya mwaka 2025 ya Jukwaa la Mtandao wa Kutokomeza ndoa za Utotoni nchini Tanzania katika mapambano dhidi ya ndoa za utotoni na vitendo vya ukatili nchini Tanzania

Licha ya kauli mbiu ya binti ni mtoto sio mke Kuhimiza mabadiriko ya Sheria ya ndoa ya mwaka 1971, lakini bado zipo baadhi ya mila na desturi zilizopitwa na wakati  zinaendelea kuwaathiri wasichana na wanawake hapa nchini.

Fuatana nami katika makala hii ya simulizi za mabinti walio na umri chini ya miaka 18 kutoka katika mkoa wa Mara, ambao wanaishi katika kituo cha nyumba salama Iliyopo Kyabakari Katika wilaya ya Butiama mkoani Mara, baada ya kukimbia familia zao kutokana na kulazimishwa kukeketwa na kutolewa huku wakiwa Watoto ambao hawajafikisha umri wa miaka 18, wakieleza magumu waliyopitia na wito wao kwa wazazi,walezi, Jamii na Viongozi  kwa ujumla.

Ripoti ya utafiti ya afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria Tanzania ya mwaka 2022, Inaonesha kuwa Mkoa wa Mara ni miongoni mwa mikoa  mitano hapa nchini, inayoongoza kwa mimba za utotoni ambapo mkoa wa Songwe ndio unaongoza kwa kuwa na asilimia 45%, ukifuatiwa na mkoa wa Ruvuma wenye asilimia 37% Katavi ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na asilimia 34%, Mkoa wa Mara ukishika nafasi ya nne ukiwa na asilimia 31%  huku mkoa wa Rukwa ukishika nafasi ya tano ukiwa na asilimia 30%


Ripoti nyingine ya utafiti ya mwaka 2024 pia inaonesha mkoa wa Mara, unashika nafasi ya tatu kwa matukio ya ukatili wa kijinsia kwa kuwa na asilimia 28, huku mikoa ya Arusha na Manyara ikiwa vinara wa matukio ya ukatili wa kijinsia kwa kuwa na asilimia 43%

Hali hii inadaiwa kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na baadhi ya mila na desturi kandamizi zilizopitwa na wakati.

Mila hizi zinaendeleza mfumo dume kwa wazazi na walezi hususani wanaume kulazimisha mabinti kuolewa kwa lengo la kujipatia mali na fedha bila kujali maamuzi ya Binti husika au mama mazazi wa binti kusikilizwa wakati wa Kufanya maamuzi,  jambo linalowaweka hatarini wasichana katika vitendo vya ukatili wa kijinsia, hali inayopelekea baadhi  hulazimika kukimbilia kwenye nyumba salama zilizopo katika wilaya za Butiama, Serengeti na Tarime na Musoma ili kutafuta hifadhi, usalama na msaada wa kisaikolojia katika masharika yanayotoa huduma hiyo.

Mabinti hawa wanaokimbia familia zao kutokana na ndoa za utotoni na uwekezaji, wanakua wanapitia changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na kutosikilizwa na kutokua na uhuru wa kufanya maamuzi na simulizi za maisha za maisha wanayopitia zinaweza kusaidia kuleta mabadiriko katika jamii kutokana na visa na mikasa wanavyokumbana navyo hadi kufanikiwa kukimbia familia zao na kwenda Kwa ndugu, jamaa au marafiki pamoja na  kufika katika vituo vya nyumba salama kutafuta hifadhi.

Hivi umewahi kufikiria mzazi anaweza kumlazimisha binti yake kuolewa ili apate ng'ombe ambazo zinatakiwa kutumika kwa mdogo wake ambaye pia yuko chini ya miaka 18 ili pia akatoe mahali ili  apate mke? Basi hiki ni kisa kimoja wapi tu Kati ya visa vingi walivyonavyo mabinti wanaoishi nyumba Salama Butiama.

Ni saa kumi na mbili na dakika hamsini jioni nafika  hapa katika kijiji cha Kyabakari  kilichopo katika wilaya ya Butiama mkoani Mara, ambapo inapatikana ofisi na kituo cha nyumba salama cha Hope For Girls and Women Tanzania, Kituo kwa ajili ya kuhifadhi wasichana waliokimbia kutoka katika familia zao ili kuepukana na ndoa za utotoni pamoja na ukeketaji kutoka Butiama na maeneo mengine ya mkoa wa Mara.

Baadhi za wilaya katika mkoa wa Mara  bado zinaonekana kuwa nyuma katika swala zima la mila na desturi ambazo zinaonekana kumkandamiza msichana na mwanamke ambapo ndoa za utotoni ni moja ya mila ambazo inaonekana kuhalalishwa na jamii ya kikurya.

Wegesa Nyamuhanga (Sio Jina lake halisi) Mwenye umri wa miaka  18 mkazi wa kijiji cha Kinyambwiga  wilaya ya Bunda Mkoani Mara, ni kati ya wasichana wanaodaiwa kuolewa  akiwa bado na umri  mdogo wakati anaishi na wazazi wake huko katika kijiji cha Kinyambwiga.

Anasema mwaka 2020, aliolewa  akiwa na umri  wa miaka 15 , Alilazimishwa kuolewa na Mama yake mzazi baada ya baba yake mazazi kufariki  kwa mahali ya ngombe 6 na kijana mwenye umri wa miaka 18.

Anasema wazazi upande wa mume walipoenda kumchumbia kwao, akakataa lakini mama yake mzazi alimlazimisha akaenda kuolewa, lakini ndoa ilimshinda akakimbia  na akamaliza mwezi mzima huko alipokimbilia lakini badae walipata taarifa nilipo wakaenda kumfuata, wakaenda ofisi ya kijiji kuendesha kesi ambapo maamuzi yalitolewa  ng”ombe warudishwe sababu alikataa kurud kwenye ndoa.

“Nilirudi kuishi nyumbani lakini mama aliendelea kunilazimisha kurudi huko nilipokua nimeolewa sababu yeye hawezi kurudisha ng’ombe, Nilivyoona mama anaendelea kunilazimisha kurudi na maisha yakawa magumu nikaona bora nitoroke nikaja hapa Butiama nikakutana na mchungaji Johanes akanipelekea kituo cha usalama jirani na mahakama wakamuita mzazi wangu lakini mimi nilikataa sirudi nyumbani ndio wakanileta hapa nyumba salama

Nilipoingia kwenye ndoa, mwanaume alikua ananipiga kila siku ananilazimisha niende shambani lakini yeye aendi, ananigombeza kila siku akawa ananichonganisha na wazazi wake anasema na tabia mbaya, mara siwajali wazazi wake kwenye chakula, nilivyoaona mateso yamezidi nikaondoka kurudi nyumbani lakini nilipofika huko mama nae akawa ananipiga ananilazimisha kurudi.

Nawashauri wazazi wasipende kuwalazimisha watoto wadogo uolewa, waache wafikishe umri mkubwa, waache kwanza watoto wasome na kutulia na familia zao” Amesema Wegesa


Ndoa za utotoni ni hali ambapo mtoto wa kike anaolewa kabla ya kutimiza umri wa miaka 18, mara nyingi bila ridhaa yake kamili na hali hiyo inapelekea kupata ujauzito katika umri mdogo kutokana na ukosefu wa elimu ya afya ya uzazi, ukatili wa kingono, au ndoa za kulazimishwa.

Kwa wasichana wadogo, hali hizi hufanyika kupitia shinikizo kutoka kwa familia, hasa kwa baba ambaye mara nyingi hutumia nafasi yake kama kichwa cha familia kuwalazimisha mabinti kuolewa kwa lengo la kupata mali – hasa ng’ombe kwa ajili ya matumizi ya familia.

Katika jamii nyingi zenye mfumo dume, maamuzi yote ya familia hufanywa na baba, huku mama na binti husika wakinyimwa haki ya kutoa maoni au kupinga maamuzi hayo. Hali hii huwanyima wasichana haki ya kupata elimu, huathiri afya yao ya mwili na akili, na kuwaweka katika mzunguko wa umasikini na utegemezi wa maisha yote.

Veronica Ryoba(sio jina lake halisi) anasema pia mwaka 2020 akiwa na umri wa miaka 13 baba yake mzazi alimlazimisha kukeketwa ili aweze kupata mahali na mahali itakayopatikana iweze kumsaidia mdogo wake wa kiume aache kusoma ili aweze kutumia mahali hiyo  kuoa.

Amesema baada ya baba yake kumuua mama yake kwa panga baada ya kurudi nyumbani na kukuta hajaachiwa chakula na baada ya tukio hilo ndipo aliamua kutoroka nyumbani baada ya kuona msada aliokua anaupata kwa mama yake haupati tena  huku baba akiendelea kumlazimisha kukeketwa ili aolewe.

“Mwaka 2020 nilikimbia ukeketaji kwa sababu baba yangu alikuaga mlevi sana na alikua anataka mimi nikeketwe ili niolewe apata mahali ambayo alitaka imsaidie mdogo wangu wa kiume aache kusoma naye aweze kuoa na kuendelea na maisha yake

Kutokana baba kuwa mlevi siku moja mama alikua hana hela ya kununua mboga baba aliporudi akiwa amelewa akamuomba mama chakula, mama akamwambia hakuna na hela ya kununu chakula ndipo baba akachukua panga na kumkata mama hadi akafariki.

Baada ya kifo cha mama niliamua kutoroka nyumbani kutokana na kukosa mtetezi ambaye alikua anatetea ni nisikeketwe na nikakimbilia kwa baba mdogo ambaye alinizaidia kunisomesha kuanzia darasa la kwanza hadi la saba na baada ya kuhitimu ndio nikakimbilia katika kituo hiki cha nyumba salama Butiama.

Nilipofika hapa nyumba salama nilipokelewa vizuri nikawaeleza changamoto nilizopitia kule kijijini, wakanisaidia kuniendeleza kielemu kuanzia kidato cha kwanza hadi nimehitimu mwaka jana kidato cha nne shule ya sekondari Kyabakari na nimefaulu na nategemea kuendelea na masomo yangu.” Anasema Veronica

Ameongeza kuwa ukatili aliofanyiwa umeathiri pakubwa maisha yake kwanza kama mzazi wake angefanikiwa kumkeketa asiwengeza kufikia malengo yake ya kumaliza elimu ya msingi na sekondari.

Kwa upande wake anatoa wito kwa wazazi na jamii kwa ujumla kuwa watetezi wa watoto wa kike maana huko maeneo ya vijijini wanaamini kuwa watoto wa kike hawawezi kuwasaidia wazazi wao na hawawezi kusoma na wanaamini kwamba mtoto wa kike akiwa amehitimu darasa la saba inatakiwa akeketwe ili aozeshwe ili awape mahali jambo ambao sio sahihi kwani nao wanahitaji kufikia malengo na kutimiza ndoto zao

Wakati Wegesa Nyamuhanga na Veronica Ryoba wakilazimishwa kuolewa na wazazi wao lakini hali ni tofauti kwa Lucia Wambura (Sio jina lake halisi) ambaye anaeleza kuwa baba yake mzazi alifariki mwaka 2020 na alikua hataki watoto wake wakeketwe lakini baada ya baba yake kufariki ndugu wa baba yake walitaka akeketwe mara baada ya kumaliza mtihani wa darasa la saba.

“Mimi kwa historia yangu nyumbani baba yetu alikua anapinga hii mila ya ukeketaji na alikua anakinzana na ndugu zake wote, sababu walikua wanafanya vitendo hivyo kwa familia zao, Kwa bahati mbaya baba yangu mwaka 2020 alifariki nikiwa darasa la tatu na baada ya hapo nilianza kufatiliwa na ndugu upande wa baba ili nikakeketwe.

Yani nilikua nataka kukeketwa mara baada ya kumaliza mtihani wa darasa la saba ila sikutaka ndipo nilipokimbia nyumbani na kukimbilia kwao na rafiki yangu ambaye tumemaliza nae darasa la saba ambapo mama yake alinipeleka dawati ambao ndio waliwailiana na huku nyumba salama ambao walinichukua na mpaka sasa naishi hapa.

Kibinafsi ni vigumu sana kutokuishi na familia yako na mimi nilizoea na nilijua siku zote ntaishi na familia yangu ila kwa sasa nipo huku nyumba salama naishi na mabinti wenzangu, Kuondoka nyumbani pia kuliathiri masomo yangu maana muda mwingine nikikaa nasoma nawaza nyumbani, nawaza kule nyumbani wanafanyaje na sio tu masomo bali hata maisha yangu ninapokaa huwa najiuliza kuhusu familia yangu na ndugu zangu wengine niliowaacha kule nyumbani.

Naishauri jamii inayoendeleza mila ya ukeketaji iachane nayo, kwa sababu inatuathiri sisi mabinti kisaikolojia na kuacha na imani potofu kuwa binti asiyekeketwa hawezi kuolewa na mwanaume ambaye sio wa kikurya hali inayomfanya binti kufikiria ni nani atakaemuoa na maisha yake ya baadae yatakuaje” Amesema Lucia.

Katika jamii ya Kikurya, mila ya ukeketaji imeendelea kuwa kichocheo kikuu cha ndoa za utotoni. Wasichana wengi hulazimishwa kufanyiwa ukeketaji wakiwa na umri mdogo, kwa madai kwamba ni njia ya kuwaandaa kutoka hatua ya utoto na kuingia kwenye utu uzima, ili wawe tayari kuolewa.

Mila hii huwasilishwa kwao kama jambo la heshima na utambulisho wa kijinsia, lakini kwa undani wake, ni mfumo wa ukandamizaji unaonyima wasichana haki ya kufanya maamuzi kuhusu miili yao na maisha yao ya baadaye. Baada ya kukeketwa, wasichana huchukuliwa kuwa tayari kuolewa, hata kama bado ni watoto kiumri na kiakili.

Wengi wao hulazimishwa kuolewa na wanaume wazee kwa lengo la familia kunufaika kwa mahari, jambo linalowatupa nje ya mfumo wa elimu na kuwaweka kwenye hatari kubwa ya madhara ya kiafya, mimba za utotoni, na ukatili wa kijinsia. Mfumo huu, unaoendeshwa na imani potofu na utawala wa mfumo dume, huwakosesha wasichana fursa ya kujiendeleza na kujenga maisha bora.

Ndoa za utotoni katika jamii ya Kikurya, msichana ambaye hajafanyiwa ukeketaji huchukuliwa kuwa bado na hafai kuolewa,  Kwa mila na desturi hizo, ukeketaji huonekana kama kipimo cha ukomavu wa msichana na hatua ya lazima kabla ya kuingia kwenye ndoa.

Rhobi Samwelly na Mkurugenzi wa shirika la Hope For Girls and Women Tanzania na Kituo cha Nyumba Salama Buatiama, anasema licha ya vitendo vya ukatili kwa watoto wa kike kupungua katika mkoa wa Mara lakini bado tatizo na mfumo dume na mila zilizopitwa na wakati viachangia tatizo hilo kuendelea kuwepo na wasichana kukimbia familia zao na kutafuta hifadhi katika nyumba salama.

Amesema kwa sasa hali ya vitendo vya ukeketaji kwa mkoa wa Mara vimepungua ikilinganishwa na miaka ya nyuma na nyumba salama za Butiama na Serengeti zimekua zikipokea mabinti wengi inapofika msimu wa ukeketaji lakini tatizo la mfumo dume bado linaonekana kikwazo kwa wasichana.

“Kwa mfano msimu wa ukeketaji uliokwisha ukiacha wa mwaka jana tuliweza kupokea watoto 480 na idadi hii ilikua ni kubwa na huko nyuma tumekua tukipokea hivyo hivyo lakini katika msimu wa ukeketaji wa 2024 nyumba zetu salama zote mbili tuliokea watoto 347" Amesema Rhobi

"Hali ya mfumo dume kwa kweli inachangia kuendelea kuwepo kwa ndoa za utotoni na mila na desturi kandamizi, kwa sababu mara nyingi katika jamii yetu baba wanasema ndio wasemaji wa mwisho na wao ndio wenye kufanya maamuzi na mwanamke hana nafasi ya kuzungumza.

Kwa mfano pale ambapo baba anapoamua binti kuolewa mara nyingi akina mama wanashindwa kuzuia maamuzi hayo maana wanamsikiliza baba akiishamaua hakuna wakupinga maamuzi yake, hali hii pia inasababishwa na mama kutokua na uchumi na kuwa tegemezi kwa baba.

Katika kuwapa elimu na kuwajengea uwezo wanawake na kuchukua hatua za kujishughulisha kiuchumi mara nyingi huwa wanawaeleza na kuuliza waume zao kwamba kwanini huyu binti yetu aolewe na asisome na wamekua wakikataa na kupinga ndoa hizo na kueleza kama ni mali basi mama atachangia kufanikisha jambo hilo hata kama ununuzi wa ng’ombe ili tu binti aendelee na masomo” Amesema Rhobi.

Baada ya kufanya mahojiano na Rhobi Samwelly, Mkurugenzi wa shirika la Hope For Girls and Women in Tanzania, ambaye alieleza kwa kina kuhusu tatizo la ndoa za utotoni na mchango wa vituo vya nyumba salama katika kusaidia wasichana wanaokimbia ukatili, nilibaki na maswali ya kujiuliza Je, ndoa hizi za utotoni zinatambulika kidini? Na je, dini inasemaje kuhusu ndoa?

Nimepata nafasi ya kuzungumza na kiongozi wa dini Sheikh Omari Ali Khamisi kutoka Masid Zanzibar Musoma, anasema ndoa kwa mujibu wa dini ya kiislamu na kwa mujibu wa sheria za dini , ndoa ni ibada na mtu anapoingia kwenye ndoa ameingia kwenye taasisi ya ibada na inaongozwa kwa kanuni zake.

Amesema mtu anaingia katika kanuni hizo anakua na mwenza wake, wakaafikiana na kushauriana kufuata kanuni kwa mujibu wa sheria ya kiislam wanakua wameingia kwenye ndoa.

“Tunapozungumzia ndoa za utotoni, tunazungumzia ndoa ambazo ziko chini ya ule umri ambao unatambulika kisheria ima kitamaduni, au sheria ya nchi au kwa madhehebu na imani tofauti tofauti.

Kwa mfano kwa mujibu wa sheria umri unaoruhusiwa mtu kuingia kwenye ndoa awe na umri za ya miaka 18 na kuendelea lakini ndoa hizi za utotoni ni pale athari za umri unapoonekana ambapo binti anakua hana fikra ya moja ya kujitegemea, hana uchumi wa moja kwa moja wa kujitegemea, anafanyiwa maamuzi na watu wengine, anaendeshewa uchumi na watu wengine.

Ili kutokomeza tatizo hili kwanza inapaswa kutolewa elimu baina ya mtu na mtu, familia, kitongoji, kijiji na maeneo mbalimbali katika jamii kuelimishana madhara yanayopatikana kuhusiana na ndoa za utotoni, madhara ya kiafya yanayopatikana na ukeketaji na ukatili wa kijinsia kwa watoto.

Tarehe 9 June, 2025 Waziri wa maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt Dorothy Gwajima Akitangaza Matokeo ya utafiti wa kitaifa wa ukatili dhidi ya watoto na Vijana ya mwaka 2024.

Alisema Matokeo ya utafiti wa Machi-Juni, 2024 yanaonesha ukatili umeshuka kwa kiwango kikubwa ukilinganisha utafiti wa 2009 ambapo,Kwa Watoto wa kike  Ukatili wa kingono umepungua kutoka 33% hadi 11%; Ukatili wa kimwili umepungua kutoka 76% hadi 24%; na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka 25% hadi 22%.

Kwa watoto wa kiume: Ukatili wa kingono umepungua kutoka 21% hadi 5%; Ukatili wa kimwili umepungua kutoka 74% hadi 21% na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka 31% hadi 16%. Na walengwa ni watoto 11,414 wenye umri wa miaka 13 hadi 24 kutoka mikoa yote 31 ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Ndoa na mimba za utotoni ni aina za ukatili wa kijinsia kwa wasichana huathiri maisha yao kwa kiwango kikubwa katika nyanja mbalimbali.

Kielimu, wasichana wengi hulazimika kuacha shule mara tu baada ya kukeketwa au kuolewa, Ki-afya, ukeketaji husababisha madhara makubwa ya kiafya yakiwemo maumivu makali, kutokwa na damu nyingi, maambukizi ya njia ya uzazi, matatizo wakati wa kujifungua, na matatizo ya afya ya akili kutokana na msongo wa mawazo na unyanyasaji wa kijinsia

Kiuchumi, ndoa za utotoni huwafanya wasichana kuwa tegemezi kwa waume zao, wakikosa ujuzi, elimu au nafasi ya kupata kipato chenye maana. Wanajikuta wakikosa uhuru wa kiuchumi na kushindwa kushiriki katika shughuli za uzalishaji mali.

Wakati hali inaonesha matukio ya ukatili kushuka lakini zipo changamoto ambazo wadau ambao ni mashirika yasiyo ya kiserikali katika mkoa wa Mara wanakumbana nazo wakati wakitekeleza majukumu yao.

Rhobi Samwelly mkurugenzi nishirika la Hope foe Girls and Women in Tanzania na Nollasko Mgimba afisa ni miradi kutoka Kanisa Katoriki Dayosisi ya Mara wanasema licha ya mafanikio yaliyopo zipo changamoto katika jamii wanapotekeleza miradi yao.

Rhobi Samwelly anasema katika kesi za ndoa za utotoni ikiwa tayari imefika katika vyombo vya haki kwa ajili ya kutoa maamuzi lakini unakuta familia zinakwamisha kwa kufanya mazungumzo nje ya vyombo hivyo vya kutoa haki na wanakubaliana ili jambo hilo lisendelee mahakamani na kupoteza ushahidi.

Amesema  pia changamoto nyingine ni vitisho na matusi toka kwa jamii ambayo bado inashikiria mila na desturi zilizopitwa na wakati huku akitoa wito kwa viongozi wa serikali na kisiasa kuendelea kutoa elimu kwa jamii.

Kwa upande wake Nollasko Mgimba anasema anasema changamoto kubwa wanayipata katika jamii wakati mwingine ni kutopokelewa na jamii kutokana na baadhi yao kuona wanapinga mila zao ambazo wengine ndio vyanzo vyao vya mapato.

Amesema changamoto nyingine ipo kwenye usimamizi wa sheria na sera zilizopo sababu jambo hili ni la kimila na viongozi wengi wanaoteuliwa au kuchaguliwa wanatoka katika mazingira hayo hayo hivyo wanakosa nguvu kubwa ya kuzisimamia sheria hizo kwa ajili ya kutokomeza ukatili huo sababu ni sehemu ya mila na desturi zao lakini pia wanahofia kuhatarisha nafasi zao na kuogopa kutochaguliwa tena na wananchi wakati wa uchaguzi.

Ametoa wito kwa wadau kushirikiana kuunganisha nguvu kwa pamoja na wadau wa maendeleo kusaidia upatikanaji wa rasilimali katika mapambano dhidi ya vitendo hivyo katika jamii.

SMAUJATA ni kampeni ya kitaifa ya kupinga ukatili wa kijinsia na ukatili kwa watoto nchini Tanzania inanyofanya kazi chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii , Jinsia, Wanawake na Makundi maalum na Joyce James ni Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa wa Mara, anasema katika mwaka huu 2025 wamepokea kesi nyingi zinazohusiana na mimba za utotoni.

Amesema ukatili wa kijinsia katika mkoa wa Mara umeendelea umeshamiri sana na katika mwaka wa 2025 wamepokea kesi nyingi za watoto kupewa mimba na kukatisha masomo yao na wengine wameachishwa masomo wakiwa hawajafikia hata elimu ya sekondari wakiwa wamepewa mimba.

“Tunayo kampeni ya kutoa elimu mashuleni ili jamii ya mkoa wa Mara iweze kutambua madhara ya ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na ndoa  na mimba za utotoni, Mfano kila shule tunayoenda kutoa elimu hasa shule za msingi tunakuta watoto wadogo ambao chini ya miaka 15 wamepewa mimba na kusitishwa masomo yao jambo ambalo linawaumiza wazazi wengi.

Tunakutana na changamoto nyingi tunazopia wakati wa kutekeleza kampeni hii mfano wazazi wengine kutotoa ushirikiano wa watukio haya lakini changamoto nyingine ni wazazi au walezi kuficha haya matukio yanayowapata watoto na sisi tunataka jamii itambue madhara ya ndoa za utotoni, Mfano wakati tunatoa elimu katika shule ya msingi Songambele iliyopo wilaya ya Musoma, walimu wameshuhudia wapo watoto ambao wamepewa mimba na kesi zao zipo katika vyombo vya sheria ili wahusika wachukuliwe hatua” Amesema Joyce James

Wanaharakati, mashirika yasiyo ya kiserikali na viongozi wa dini wamekua wakipendekeza mabadiriko ya Sheria ya ndoa ya  mwaka 1971  hususani kwenye vifungu vya 13 na 17 vinavyoruhusu mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 14 na 15 kuolewa kwa ridhaa ya wazazi au kwa amri ya mahakama kwa madai kwamba  Sheria hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo ni pamoja na; kuruhusu mazingira fulani ya ubaguzi wa kijinsia kwa wanawake na wasichana , kuimarisha elimu na uhamasishaji wa jamii katika kukomesha tatizo la ndoa za utotoni .

Rebecca Gyumi ni Mkurugenzi wa Shirika la Msichana Initiative, ambaye ni miongoni mwa wanaharakati nchini Tanzania, alifungua kesi Mahakama Kuu ya Tanzania kwa niaba ya watoto wote walio katika hatari ya kuingia kwenye ndoa za utotoni dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa serikali la madai namba tano(5) ya mwaka 2016 kupinga uhalali wa kikatiba wa ndoa za utotoni.

Wakati wanaharakati hao kupitia Mtandao wa Kumaliza Ndoa za Utotoni Tanzania (TECMN) wakisubiri Serikali kutekeleza hukumu hiyo, Mnamo Mei 10, 2025 Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Damas Ndumbaro katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dodoma  alinukuliwa akisema baadhi ya ndoa zinagusa imani za watu.

“Baadhi ya ndoa zinagusa maisha ya watu hivyo huwezi kubadilisha imani hizi kwa kutunga au kurekebisha sheria bila kwanza kushauriana na kupata ridhaa ya watu hawa, na ridhaa haiwezi kulazimishwa. Serikali imeelekezwa na mahakama, lakini kumbuka, lazima tupate ridhaa ya watu wote hawa.” Alisema Dkt Ndumbaro

Baada ya kauli ya Mhe. Dkt Damas Ndumbaro, Mtandao wa Kumaliza Ndoa za Utotoni Tanzania pia ukaja na wito wa kuiomba serikali iharakishe mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 kama ilivyoelekezwa kwenye kesi ya Rebeca Gyumi. Vilevile, tunatoa wito wa kufanyika kwa marekebisho ya sheria nyingine zote zinazowanyima wasichana haki zao, ili kuimarisha ulinzi wa watoto wa Tanzania

Wakieleza kutambua kuwa mila na imani za kidini ni sehemu ya utambulisho wa jamii, tunasisitiza kwa nguvu zote kuwa haki za watoto haziwezi kuwa kafara ya mila au tafsiri za kidini ambazo zinawaweka watoto hasa wasichana katika hatari ya ndoa za utotoni ambazo zina madhara makubwa kiafya, kielimu, kiuchumi, na kisaikolojia.

“Mtandao wa kutokomeza ndoa za utotoni Tanzania kama wadau wa haki za watoto tumesikitishwa na kauli iliyotolewa na Waziri wa katiba na Sheria Dkt Damas Ndumbaro siku ya tarehe 10/5/2025  wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dodoma.

Wakati wote kunapokua na mgangano kati ya dini,mila na sheria, sheria ndio utawala na kutumika kwa sababu sheria ndio inayoleta usawa, na dini zipo tofauti kuna wengine wakristo, wengine waislam na kuna wengine hawana dini kabisa hivyo ni vigumu kusema utashi wa dini ndio uongoze maslahi ya watu wote” Wanajukwaa la TECMN

Wakati dunia ikiadhimisha siku 16 za Uanaharakati  kwa kauli mbiu madhubuti ya kupinga na kutokomeza ukatili kijinsia ukatili dhidi ya mwanamke na mottomwaka  2024 isemayo Kuelekea Miaka 30+ ya Beijing: Chagua Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia lakini bado baadhi ya maeneo nchini ikiwa ni pamoja na mkoa wa Mara yanaonekana kutotekeleza kwa vitendo kauli hiii.



 



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top